Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, June 14, 2014

Mapigano katika mpaka wa Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo

Maafisa wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo juzi Alkhamisi walitangaza habari ya kutokea mapigano kati ya askari jeshi wa nchi hiyo na Rwanda katika mpaka wa pamoja wa nchi hizo jirani. Walisema mapigano hayo yalipelekea kuuawa kwa askari watano wa Kongo. Mapigano mengine kama hayo yaliyojiri siku ya Jumatano yalipelekea askari wengine kadhaa kuuawa na kujeruhiwa. Maafisa wa nchi hizo wamekuwa wakituhumiana na kunyoosheana vidole kuhusiana na msababishaji hasa wa kuongezeka mvutano katika mpaka wao wa pamoja.
Julien Kahongya Paluku, Gavana wa Jimbo la Goma, makao makuu ya Kivu Kaskazini, mashariki kwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo amewatuhumu askari wa Rwanda kuwa ndio walioanza kuwafyatulia risasi wenzao wa Kongo, na kuongeza kuwa askari wa Kongo wametakiwa kujizuia kujibu mashambulio ya askari wa Rwanda kadiri wanavyoweza.
Kwa upande wao maafisa wa Rwanda wanasema kuwa mashambulio ya askari wa DRC katika ardhi yao ni jambo la kawaida na kuwa huwa wanavuka mpaka na kuingia katika ardhi ya Rwanda kwa lengo la kuwinda wanyama wa porini. Hata hivyo wanasema katika matukio ya hivi karibuni hawakuwafyatulia risasi wanyama tu bali waliwafyatulia pia risasi askari wa Rwanda. Wakazi wa miji ya mpakani ya Rwanda pia wamesema kuwa askari hao wa Kongo walianza kufyatuliana risasi na askari wa Rwanda walipoingia katika ardhi ya nchi hiyo kwa lengo la kuiba mifugo.
Akizungumzia mapigano hayo, Martin Kobler, mkuu wa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo amezitaka pande mbili hizo kuwa na subira na kufanya juhudi za kurejesha amani na utulivu katika mpaka wao wa pamoja. Maafisa wa kimataifa wanatumai kwamba pande mbili hizo zitaheshimu na kutekeleza kikamilifu Mkataba wa Amani, Usalama na Ushirikiano katika eneo la Maziwa Makuu uliotiwa saini tarehe 24 Februari mwaka uliopita huko Addis Ababa Ethiopia.
Baadhi ya wachambuzi wa mambo wanasema kuwa chanzo hasa cha mapigano na mivutano katika mpaka wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Rwanda ni uungaji mkono wa Kongo kwa waasi wa FDLR wa Rwanda ambao wana kambi zao katika ardhi ya nchi hiyo. Waasi hao ambao ni wa kabila la Hutu wanatuhumiwa na serikali ya Kigali kwamba wanafanya njama za kuzusha ghasia na machafuko huko Rwanda. Waasi hao walihusika pakubwa katika mauaji ya kimbari ya 1994 nchini Rwanda, mauaji ambayo yalidumu kwa muda wa zaidi ya miezi mitatu na kupelekea watu laki nane kupoteza maisha yao. Hii ni katika hali ambayo wajuzi wengine wa mambo wanasema kuwa mapigano ya hivi karibuni yamechochewa na Rwanda kwa lengo la kulinda maslahi yake katika eneo hilo. Nchi hiyo imekuwa ikituhumiwa na Umoja wa Mataifa kwamba inawapa silaha waasi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwa lengo la kupora madini ya nchi hiyo. Rwanda na Uganda zimekuwa zikituhumiwa kuingilia mambo ya ndani ya Kongo kwa sababu mbalimbali na hasa ya kupora maliasili za nchi hiyo.

No comments: