Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, June 14, 2014

Njama za wapinzani kwa ajili ya kuzusha machafuko nchini Mauritania

Rais Mohamed Ould Abdel Aziz wa Mauritania juzi Alkhamisi, aliwatuhumu wapinzani wa serikali yake kuwa wanafanya njama za kuzusha machafuko ndani ya nchi hiyo. Katika wiki za hivi karibuni, wapinzani wamekuwa wakifanya maandamano ya mara kwa mara sambamba na kutoa nara dhidi ya serikali ya Nouakchott na kutaka kususiwa uchaguzi ujao wa rais uliopangwa kufanyika tarehe 21 ya mwezi huu wa Juni. Hii ni katika hali ambayo vyama vya upinzani, sanjari na kuhoji juu ya uhalali na mwenendo wa uchaguzi huo, vimekituhumu chama tawala kwa kufanya njama za kuiba na kubadili matokeo ya uchaguzi huo.
Makundi ya upinzani yanasema hatua ya kutangazwa tarehe ya uchaguzi na upande mmoja tu ni njama ya serikali ya kutaka kufanya uchakachuaji katika uchaguzi. Wakati huo huo, Rais Ould Abdel Aziz amesema njama za wapinzani za kutaka kuingia madarakani kwa nguvu zitaambulia patupu. Rais Ould aliyasema hayo katika mkutano mmoja wa kampeni za uchaguzi mjini Nouakchott. Aidha rais huyo sambamba na kuwatuhumu wapinzani kwa uongo, amesema watu wanaopanga kususia uchaguzi kuwa ni mabaki ya utawala mbovu uliopita na kuwataka wafuasi wake wahudhurie kwa wingi katika uchaguzi huo. Ould Abdel Aziz ambaye pia ni jenerali wa zamani wa jeshi, atachuana na wagombea wanne akiwemo mwanamke mmoja katika kutetea kiti chake cha urais. Kuna wasi wasi kwamba, uchaguzi huo huenda ukavuruga hali ya mambo nchini Mauritania. Jumuiya ya Kidemokrasia na Umoja ambao ni muungano wa wapinzani nchini humo, sambamba na kutoa tamko imetangaza kuwa, hakuna dhamana yoyote inayohakikisha kuwa uchaguzi huo wa rais utafanyika kwa uhuru na haki au kuufanya uonekane kuwa na itibari. Ni kwa ajili hiyo ndio maana muungano huo, ukayataka makundi mengine kususia uchaguzi huo. Mbali na hayo wapinzani pia wametangaza azma yao ya kufungamana na mazungumzo na serikali. Hata hivyo wamedai kuwa, viongozi wa chama tawala hawako jaddi kuendelea na mazungumzo kwa lengo la kuukwamua mzozo wa nchi hiyo. Rais Mohamed Ould Abdel Aziz ambaye aliingia madarakani kupitia mapinduzi ya kijeshi, sanjari na kuitisha uchaguzi wa mwaka 2009, amejitahidi kuhakikisha utawala wake unatambuliwa kisheria. Hii ni katika hali ambayo wapinzani wa Mauritania wanaitaja hatua hiyo kuwa ni hila kwa ajili ya kupora madaraka ya taifa hilo. Kwa miaka yote ya hivi karibuni, utawala wa Rais Ould Abdel Aziz umekuwa ukishuhudia maandamano na malalamiko ya wananchi. Vitendo vya udikteta na kuwekewa mibinyo watu maalumu kwa upande mmoja na kadhalika kushindwa kuimarisha hali ya usalama nchini kwa upande mwingine, kumepunguza uungaji mkono wa wananachi kwa rais huyo. Vitendo vya kigaidi katika miaka iliyopita, ni jambo jingine ambalo limeathiri usalama wa taifa hilo. Mbali na suala la usalama, kukosekana ridhaa ya kisiasa nchini Mauritania, umasikini na ubaguzi uliokita mizizi, ni mambo mengine ambayo yamezusha hali ya mchafukoge ndani ya nchi hiyo.

No comments: