Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Friday, May 16, 2014

Pendekezo la kuufanyia marekebisho muundo wa Tume ya Uchaguzi ya Ivory Coast

Hamed Bakayoko, Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ivory Coast ametoa pendekezo jipya  la kufanyiwa marekebisho muundo wa Tume Huru ya Uchaguzi ya nchi hiyo. Kwa mujibu wa muundo wa awali, idadi ya wajumbe wa tume hiyo ilikuwa 31 na inapasa kupunguzwa ambapo idadi ya wawakilishi wa chama tawala ilikuwa mara mbili ya wawakilishi ya vyama vya upinzani. Kwa upande wa serikali, licha ya kuwepo wawakilishi watatu kutoka chama tawala, kulikuwa na wawakilishi wengine wanne ambapo mmoja anateuliwa na Rais, na wengine waliosalia wanatoka Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Uchumi na mwingine kutoka baraza kuu la sheria la nchi hiyo.
Hii ni katika hali ambayo, mrengo wa upinzani na ule wa jumuiya za kiraia zilitengewa nafasi tatu kila moja. Kwa muda mrefu sasa mrengo wa upinzani umekuwa ukilalamikia muundo huo ambao umekuwa ukikipatia nguvu zaidi chama tawala. Suala la kuvunjwa tume huru ya uchaguzi nchini Ivory Coast ambayo ilitekeleza jukumu la kuendesha uchaguzi wa rais wa 2010, uchaguzi wa bunge wa 2011 na uchaguzi wa  mabaraza ya miji na serikali za mitaa wa 2013, ni miongoni mwa matakwa yaliyotolewa na  wapinzani nchini humo. Hii ni katika hali ambayo, Chama cha Demokrasia, ambacho kinamuunga mkono Rais Alassane Ouattara kimewatuhumu wapinzani kwamba wanang'ang'ania mambo yasiyo na msingi wowote. Inaonekana kuwa, serikali ya Ivory Coast imeamua kulegeza misimamo yake ya awali na kuliangalia upya pendekezo la kufanyiwa marekebisho tume hiyo. Kwa mujibu wa pendekezo jipya lililotolewa na Waziri Hamed Bakayoko, Tume ya Taifa ya Uchaguzi itakuwa na jumla ya wajumbe 17, ambapo itakuwa na mwenyekiti, wajumbe wanne kutoka serikalini, wajumbe wanne kutoka chama tawala, wanne kutoka jumuiya za kiraia na wengine wanne watatoka kambi ya upinzani. Pendekezo hilo la serikali la kuifanyia marekebisho tume ya uchaguzi, litawasilishwa bungeni tarehe 19 mwezi huu. Muundo wa tume ya uchaguzi ulikuwa mwiba na mzozo mkubwa kati ya kambi ya wapinzani na serikali ya Ivory Coast. Weledi wa mambo wanasema kuwa, muundo mzuri na usioegemea upande wowote, utazuia kukaririwa machafuko kama yale yaliyotokea mwaka 2010 baada ya kufanyika uchaguzi wa rais. Licha ya weledi hao wa masuala ya kisiasa, Umoja wa Mataifa uliwahi kusisitiza juu ya kufanyiwa marekebisho muundo wa tume ya uchaguzi ili kuepusha kujitokeza tena machafuko nchini Ivory Coast. Baadhi ya weledi hao wanasema kuwa, muundo uliopita wa tume ya uchaguzi ulitoa mwanya kwa tume hiyo kudhibitiwa na chama tawala ikilinganishwa na pendekezo jipya la serikali. Imeelezwa kuwa, uchaguzi wa rais umepangwa kufanyika mwezi Oktoba mwakani. Weledi wa mambo wanasema kuwa, kipindi kilichosalia hadi kufanyika uchaguzi huo ni muhimu mno kwa wanasiasa na wananchi wa Ivory Coast, na hasa ikizingatiwa kwamba migogoro mingi ilijitokeza nchini humo wakati wa kipindi cha uchaguzi. Wachambuzi wa mambo wanaamini kwamba, marekebisho ya muundo wa tume ya uchaguzi pekee hayataweza kuwa na taathira kubwa ya kuzuia kukaririwa tena mapigano yaliyotokea miaka iliyopita ambayo yalisababisha mamia ya maelfu ya watu kuuawa na kuwa wakimbizi. Wachambuzi wengine wanasema kuwa, kutolewa mafunzo ya uraia na misingi ya demokrasia na hasa mashuleni na hali kadhalika  kukomeshwa uingiliaji wa madola ya kigeni nchini Ivory Coast, ni miongoni mwa mambo yanayoweza kudhamini  amani na utulivu  nchini humo.

No comments: