Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Friday, May 16, 2014

Uchaguzi wa rais Misri, ahadi za wagombea na maandamano

Wamisri waishio nje ya nchi leo wameendelea kupiga kura katika uchaguzi wa rais ikiwa ni siku ya pili tokea zoezi hilo lianze siku ya Alkhamisi. Kuna wagombea wawili tu katika uchaguzi wa rais nchini Misri ambao wangali wanaendeleza kampeni zao huku wafuasi wa Harakati ya Ikhwanul Muslimin wakisema uchaguzi huo ni kinyume cha sheria. Wamisri waishio nje ya nchi wataendelea kupiga kura hadi kesho Jumamosi. Kuna vituo 141 vya kupigia kura katika nchi 124 duniani ambapo Wamisri wanaokadiriwa kushiriki katika zoezi hilo ni laki sita.
Kabla ya kuanza zoezi la upigaji kura nje ya nchi, serikali iliondoa masharti magumu ya wale wanaoweza kujisajili kwa ajili ya kupiga kura na ndio maana inatazamiwa kuwa idadi ya wapiga kura itaongezeka. Uchaguzi wa rais ndani ya Misri unatazamiwa kufanyika Mei 26 na 27 ambapo wagombea wawili wanaowania kiti cha urais ni mkuu wa zamani wa jeshi Abdul Fattah el-Sisi na mwanasiasa wa mrengo wa kushoto Hamdeen Sabahi. El-Sisi ambaye alikuwa waziri wa ulinzi alikuwa na nafasi muhimu katika kuondolewa madarakani Muhammad Morsi, rais aliyekuwa amechaguliwa kwa njia halali. Morsi ni mwanachama mwandamizi wa Harakati ya Ikhwanul Muslimin. Siku chache zilizopita katika kampenzi zake za uchaguzi, el-Sisi alisema akichaguliwa atahakikisha kuwa Harakati ya Kiislamu ya Ikhwanul Muslimin inafutwa kikamilifu katika medani ya kisiasa Misri. Naye Hamdeen Sabahi amesema akichaguliwa atazingatia zaidi masuala ya sera za kigeni ambapo amesisitizia ulazima wa kubadilisha vipengee vya mkataba wa Camp David kati ya Misri na utawala wa Kizayuni na pia kusitisha msaada wa kifedha wa Marekani kwa Misri. Huku hayo yakijiri wapinzani wameshiriki katika maandamano dhidi ya serikali ya mpito na zoezi zima la uchaguzi wa rais. Wafuasi wa harakati ya Ikhwanul Muslimin leo Ijumaa asubuhi wameandamana mbele ya Masjidul Istiqama katika medani kuu ya mji wa Giza. Katika maandamano hayo wametoa nara dhidi ya makamnada wa jeshi na polisi.
Waandamanaji na wapinzani wanaamini kuwa, uchaguzi wa sasa wa rais nchini Misri si halali kwani Muhammad Morsi alipinduliwa baada ya kuwa rais wa kwanza kuchaguliwa kwa njia ya demokrasia Misri baada ya kutimuliwa dikteta Hosni Mubarak. Wapinzani wanasema baada ya kupinduliwa serikali halali ya Morsi, uchaguzi wa sasa wa rais ni hatua ya jeshi kutwaa tena madaraka na kuirejesha Misri katika hali iliyokuwa nayo kabla ya mapinduzi ya wananchi ya Februari 25 mwaka 2011.Ni kwa sababu hiyo ndio maana 'Harakati ya Aprili 6' nayo pia ikajiunga na wapinzani wanaosusia uchaguzi wa rais. Mratibu wa harakati hiyo, Amru Ali amesema kile kinachojiri si uchaguzi bali ni zoezi la uteuzi wa kumfanya Abdul Fattah el-Sisi awe rais wa Misri. Hali ya hivi sasa Misri inaashiria ukweli huu kuwa, uchaguzi wa rais si tu hautasaidia kurejesha utulivu nchini humo bali uchaguzi huo utazidisha ghasia na machafuko katika nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika.

No comments: