Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, May 31, 2014

Maandalizi ya serikali ya Mali ya kufanya mazungumzo na wapinzani

Waziri Mkuu wa Mali ameeleza kuwa serikali yake imejiandaa kufanya mazungumzo na makundi ya wapinzani wenaobeba silaha huko kaskazini mwa nchi. Moussa Mara sambamba na kukaribia kuanza kwa mazungumzo hayo, ameelezea pia matarajio yake ya kuhitimishwa mapigano huko mjini Kidal. Makubaliano ya usitishaji mapigano yalifikiwa wiki iliyopita huko mjini Kidal kati ya mwakilishi wa serikali ya Bamako na makundi matatu ya wapinzani chini ya usimamizi wa Umoja wa Afrika AU, hata hivyo hadi sasa bado hayajatekelezwa.
Katika kikao cha wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kilichoitishwa kwa lengo la kujadili hali ya mambo nchini Mali, washiriki walizitaka pande mbili kutekeleza haraka makubaliano hayo ya usitishwaji mapigano. Katika sehemu ya makubaliano hayo ambayo yalijumuisha vipengee vinavyohusu ubadilishanaji mateka na kuwasilisha misaada ya kibinaadamu kwa wakimbizi, kulisisitiziwa pia kuanza mazungumzo ya pande mbili. Ni kwa ajili hiyo ndio maana weledi wa mambo wakawa na matumaini ya kuwepo uwezekano wa kukaa pamoja pande husika hasa kwa kuzingatia makubaliano yaliyofikiwa kati ya mwakilishi wa serikali na makundi matatu ya upinzani ambayo ni Harakati ya Ukombozi wa Azawad, Baraza Kuu la Umoja wa Azawad na Harakati ya Kiarabu ya Wazawa wa Azawad. Pamoja na yote hayo, kuwepo tofauti kati ya makundi hayo matatu yenye mafungamano na kabila la Tuareg linalopigania kujitenga eneo la kaskazini mwa nchi hiyo, kunaweza kupelekea kuahirishwa mazungumzo hayo tarajiwa ya amani. Makubaliano ya mjini Ouagadougou, Burkina Faso yaliyofikiwa mwezi Juni mwaka jana chini ya upatanishi wa nchi hiyo, yalisisitizia pia juu ya udharura wa kufanyika mazungumzo kuhusiana na mgogoro wa nchi hiyo. Kwa mtazamo wa weledi wa mambo, mashirikiano ya nchi za eneo la Sahel la Afrika na halikadhalika juhudi za nchi za magharibi mwa bara hilo katika kuharakisha mwenendo wa amani na mazungumzo ya kitaifa kuhusiana na mgogoro wa kaskazini mwa taifa hilo, yanatajwa kuwa yenye taathira kubwa katika kadhia hiyo. Mbali na hayo mwaka jana katika kikao cha wakuu wa nchi za Jumuiya ya Kiuchumi ya Magharibi mwa Afrika ECOWAS kilichofanyika mjini Yamoussoukro, Côte d'Ivoire, sanjari na kukaribisha makubaliano ya amani, wakuu hao walitaka kutekelezwa makubaliano hayo ya amani. Kabla ya hapo pia viongozi wa nchi za eneo la Sahel la Afrika hapo mwezi Januari mwaka jana walisisitizia juu ya udharura wa kudhaminiwa usalama wa eneo hilo. Ni wazi kwamba ushirikiano wa askari wa kulinda amani wa kimataifa kwa kushirikiana na jeshi la Mali katika juhudi za kuyanyang’anya silaha makundi ya upinzani, kurejea katika hali ya kawaida maisha ya wananchi, kulindwa umoja wa kitaifa na umoja wa jeshi la nchi hiyo, ni mambo yenye umuhimu mkubwa katika kusaidia kumaliza hali ya mchafukoge nchini humo. Hatua ya Waziri Mkuu wa Mali Moussa Mara ya kutangaza utayarifu wa serikali yake kwa ajili ya kuanza mazungumzo na makundi ya wapinzani wa serikali ya Bamako, inakuja kufuatia uungaji mkono wa kisiasa wa nchi jirani na taifa hilo hasa Côte d’Ivoire na Burkina Faso. Aidha utayarifu huo na sisitizo la serikali ya Moussa Mara, kwa ajili ya mazungumzo hayo, limezingatia ukweli huu kwamba hivi sasa viongozi wa nchi za eneo la magharibi mwa Afrika, wamefikia natija hii kwamba, mgogoro wa kaskazini mwa Mali unaweza kutatuliwa tu kwa njia za kidiplomasia. Hivyo katika kikao cha kujadili hali ya usalama wa nchi hiyo kitakachofanyika wiki ijayo mjini Bamako, viongozi wa serikali pia watajadili makubaliano yaliyofikiwa hivi karibuni na wapinzani. Na ikiwa wapinzani watatoa jibu chanya kuhusiana na pendekezo la Waziri Mkuu wa nchi hiyo, basi mazungumzo ya amani yatafanyika katika anga chanya.

No comments: