Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, May 31, 2014

FDLR yatoa masharti ya kukabidhi silaha Rwanda

Waasi wa kundi la FDLR nchini Rwanda walioko mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wamekubali mpango wa kupokonywa silaha kwa sharti wafanye mazungumzo na serikali ya Kigali. Taarifa zinasema kuwa, waasi hao wameeleza kwamba, suala la kupokonywa silaha ni mwanzo wa harakati za kurejeshwa amani na utulivu katika eneo la Maziwa Makuu ya Afrika. Hata hivyo, waasi hao FDLR wamesisitiza kwamba, mpango huo unaweza kufanikiwa iwapo viongozi wa serikali ya Rwanda nao watakubali kufanya mazungumzo ya amani na waasi hao wa Kihutu.
Hivi karibuni, waasi hao waliamua kuweka chini silaha zao na badala yake wakatangaza azma yao ya kutumbukia kwenye uwanja wa kisiasa nchini Rwanda. Hayo yanaelezwa katika hali ambayo, siku chache zilizopita wanamgambo wapatao 100 kundi hilo waliweka silaha zao chini kwenye sherehe zilizofanyika katika jimbo la Kivu Kaskazini. Jenerali Victor Byiringiro Kamanda wa wanamgambo wa FDLR amesema kuwa, hatua hiyo imechukuliwa kwa shabaha ya kuonyesha nia njema waliyokuwa nayo, na kuiomba jamii ya kimataifa kutekeleza majukumu yao ya kuandaa mazingira ya kufanyika mazungumzo ya amani kati ya pande hizo mbili. Imeelezwa kuwa sherehe hiyo ilihudhuriwa na baadhi ya makamanda wa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa nchini Kongo MONUSCO.

No comments: