Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, May 31, 2014

Matamshi ya Bashar al Jaafari kuhusu msimamo wa Baraza la Usalama kuhusiana na Syria

Mwakilishi wa kudumu wa Syria katika Umoja wa Mataifa amelaumu msimamo wa Baraza la Usalama la umoja huo kuhusiana na magaidi wanaofanya mauaji nchini mwake. Bashar al Jaafari amesema, baadhi ya nchi wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wanayaunga mkono kwa uwazi na kwa siri makundi ya kigaidi na ndiyo maana makundi hayo yanaendelea kufanya jinai huko Syria. Amesema, nchi hizo zinaunga mkono vitendo vya kigaidi nchini Syria kwa kutumia nadharia ya kwamba "lengo linahalalisha njia." Amesema nchi hizo zimeamua kutumia njia yoyote ile kufikia malengo yao ya kisiasa hata kama njia hizo zitapelekea kuuawa maelfu ya wananchi wa Syria.
Mwakilishi wa kudumu wa Syria katika Umoja wa Mataifa ametoa mfano akisema, kukatiwa maji zaidi ya wakazi milioni tatu wa mji wa Halab na kuvurumishwa makombora kwenye mashule, Vyuo Vikuu na mikutano ya uchaguzi ya wananchi katika mkoa wa Dar'a ni matokeo ya uungaji mkono wa baadhi ya wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa magenge ya kigaidi huko Syria. Matamshi hayo ya Bashar al Jaafari yamekuja katika hali ambayo Umoja wa Ulaya umeamua kuongeza vikwazo vyake dhidi ya Syria hadi mwezi Juni 2015 kutokana na serikali ya nchi hiyo kuamua kuwapa haki yao ya kidemokrasia wananchi wa nchi hiyo ya kuchagua kiongozi wanayemtaka.  Baadhi ya duru zimesema kuwa, hatua hiyo ya kindumilakuwili ya Umoja wa Ulaya imechukuliwa ili kukwamisha kufanyika uchaguzi huko Syria. Ni jambo lisilo na shaka kwamba mgogoro wa hivi sasa wa Syria unatokana na siasa za kupenda vita za baadhi ya nchi za Magharibi pamoja na Marekani. Baadhi ya nchi za eneo la Mashariki ya Kati na jirani na Syria nazo zinashutumiwa kushirikiana na Marekani katika jinai zinazofanywa dhidi ya wananchi na maafisa wa serikali nchini Syria. Mtandao wa Intaneti wa Horriyat wa nchini Uturuki umeripoti kuwa, katika mkakati mpya wa Rais Barack Obama wa Marekani, makundi ya kigaidi yatakuwa yanapewa mafunzo ya kijeshi nchini Uturuki. Mtandao huo umemnukuu Ahmad Davoudoglu, Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki akisema kuwa, kuna matukio muhimu sana yatashuhudiwa karibuni hivi nchini Syria. Matamshi hayo yakipimwa na sisitizo la Obama la kusema kuwa atashirikiana zaidi na Uturuki kuhusu kadhia ya Syria na wakati huo huo Rais huyo wa Marekani akatangaza kuongeza misaada yake kwa waasi wa Syria, yanafafanua makusudio ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki kuhusu matukio muhimu yatakayotokea karibuni hivi nchini Syria. Duru za habari zimefichua pia kuwa, hadi hivi sasa Marekani imeshatumia dola milioni laki tatu kuyasaidia magenge ya kigaidi yanayofanya mauaji nchini Syria. Nchi za Saudi Arabia, Qatar, Imarati pamoja na Uturuki zinatajwa kuwa ni miongoni mwa nchi ambazo zinayasaidia sana magenge ya kigaidi nchini Syria lengo likiwa ni kutaka kuvuruga uchaguzi wa rais huko Syria. Hata hivyo, wananchi wa Syria walioko nje ya nchi hiyo wamejitokeza kwa wingi sana katika uchaguzi huo jambo ambalo linahesabiwa kuwa ni jibu la wazi la upinzani wa wananchi hao kwa magenge ya kigaidi na mabwana zao na uungaji mkono wao mkubwa kwa jitihada za serikali yao ya Syria za kupambana na magenge ya kigaidi.

No comments: