Siku ya Jumatatu ya Novemba 25 mwaka huu, ilisadifiana na siku ya
kimataifa ya kupambana na ukandamizaji dhidi ya wanawake duniani.
Sherehe hizo zilifanyika sambamba na kuwakumbuka wasichana watatu raia
wa nchi ya Jamhuri ya Dominica maarufu kwa jina la akina dada wa
“Mirabal” waliouawa na vibaraka wa utawala wa kidikteta wa nchi hiyo
mnamo tarehe 25 Novemba mwaka 1960, baada ya kupigwa vibaya,
kudhalilishwa na kutukanwa. Tuhuma zilizokuwa zikiwakabili wanawake hao
watatu ni kushiriki katika harakati za kisiasa dhidi ya utawala wa
wakati huo nchini humo.
Ni kufuatia tukio hilo na baada ya ombi la
mashirika kadhaa na wanaharakati wa kutetea haki za binaadamu duniani,
ndipo mwaka 1999 Umoja wa Mataifa ukaitangaza rasmi tarehe 25 Novemba
kuwa siku ya kimataifa ya kupambana na ukandamizaji dhidi ya wanawake
duniani. Tangu mwaka huo siku hiyo imekuwa ikiadhimishwa kimataifa na
nchi kadhaa za dunia kuwasilisha mipango mbalimbali ya kupambana na
ukandamizaji huo.
Neno ‘ukandamizaji dhidi ya wanawake’ ni istilahi maalumu ambayo
hutumika katika kuelezea vitendo vya unyanyasaji dhidi ya wanawake.
Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa limeuarifisha unyanyasaji unaofanywa
dhidi ya wanawake kuwa ni, “kila kitendo cha unyanyasaji wa kijinsia
ambacho kinaweza kusababisha madhara ya kimwili, kijinsia au
kisaikolojia kwa wanawake.” Hata hivyo suala la kusikitisha ni kwamba,
hadi sasa hakuna hatua madhubuti zilizochukuliwa katika ulimwengu wa leo
katika kuzuia vitendo hivyo, licha ya baadhi ya nchi za dunia kujinadi
kupambana na ukandamiza huo dhidi ya wanawake. Suala hilo limepelekea
hata baadhi ya viongozi wa Umoja wa Mataifa akiwemo Ban Ki-moon Katibu
Mkuu wa umoja huo, kukosoa kile kilichotajwa kuwa ni tofauti iliyopo
kati ya maneno na utendaji katika kupambana na ukandamizaji dhidi ya
wanawake na wasichana duniani.
Hadi sasa tukiwa katika milenia ya tatu vitendo vya ukandamizaji
dhidi ya wanawake vimezidi kushika kasi. Katika maeneo kadhaa
ulimwenguni, vitendo hivyo hutendeka kwa njia tofauti ukiwemo,
unyanyasaji na utumwa wa ngono, unyanyasaji wa maneno, unyanyasaji
unaotokana na vita, unyanyasaji wa kimpangilio, unyanyasaji wa miamala
mibovu na unyanyasaji wa kisiasa. Hii leo unyanyasaji dhidi ya wanawake
umekithiri sana katika nchi za Magharibi hususan Marekani. Hii ni katika
hali ambayo serikali ya nchi hiyo imekuwa ikizituhumu serikali za nchi
nyingine zinazopinga siasa zake kuwa zinawakandamiza wanawake. Hata
hivyo taasisi za wananchi wa Marekani zinaripoti kuwa, vitendo hivyo
vimeongezeka kwa kiasi kikubwa nchini humo. Moja ya vitendo vibaya vya
ukandamizaji huo ni pamoja na unyanyasaji wa kijinsia na ufisadi wa
kiakhlaqi vilivyotawala nchini Marekani. Kituo cha kukabiliana na
migogoro ya unyanyasaji cha Santa Barbara nchini Marekani kimeandika
ripoti kama ninavyonukuu: “Katika kila dakika 1.3 mwanamke mmoja wa
Kimarekeni hukumbwa na unyanyasaji wa kijinsia na vitendo vyote hivyo
hutelekezwa kikatili.” Mwisho wa kunukuu. Nayo taasisi ya Marekeni ya
‘RAINN’ ambayo inajihusisha na uchunguzi wa vitendo vya unyanyasaji,
mateso na uhusiano haramu kati ya familia na jamaa, imethibitisha ripoti
hiyo na kuongeza kuwa watendaji wa jinai hizo za kijinsia hawatiwi
mbaroni wala kufungwa jela. Ukweli ni kwamba, kutokana na serikali ya
Marekani kushindwa kuwachukulia hatua kali wahusika wa vitendo hivyo,
jambo hilo limewapa ujasiri wahalifu kuendelea na jinai zao hizo.
Umoja wa Ulaya pia licha ya kupiga hatua kubwa za maendeleo ya
kimaada, umeshindwa kabisa kuwalinda wanawake kutokana na ujangili huo
wa kijinsia. Idadi kubwa ya wanawake wanaokumbwa na unyanyasaji wa
kijinsia, kimwili na kisaikolojia katika familia za Ulaya imekuwa ni ya
kutia wasiwasi. Kwa mujibu wa ripoti ya Umoja huo, licha ya kuwekwa
sheria kali za kuzuia unyanyasaji wa kifamilia dhidi ya wanawake barani
humo, lakini vitendo hivyo vimezidi kuongezeka katika ngazi zote siku
hadi siku. Kwa mfano nchini Uingereza tu, karibu kila dakika moja
mwanamke mmoja huipigia simu polisi akiripoti kutendewa ukandamizaji
katika familia yake. Aidha wanawake wa nchi nyingine za Ulaya nao
hawajanusurika na ukandamizaji huo wa kifamilia dhidi yao. Baadhi ya
nchi kama vile Sweden, Ujerumani, Ufaransa, Uhispania, Ubelgiji, Ureno,
Uholanzi, Uguriki na Serbia, kunaripotiwa ongezeko kubwa la vitendo vya
ukandamizaji wa kimwili na miamala mibaya dhidi ya wanawake. Kwa mfano
tu nchini Italia kunaripotiwa kwamba, katika kila siku tatu mwanamke
mmoja huuawa huku nchini Serbia kukisemekana kwamba asilimia 82 ya
vitendo vya unyanyasaji wa kimwili dhidi ya wanawake hufanyika majumbani
ambapo vingi hutekelezwa kwa kutumia silaha kama vile bastola na visu.
Kwa mujibu wa baadhi ya ripoti karibu nusu ya wanawake wote walio
ndani ya ndoa huko nchini India nao pia wanakabiliwa na vitendi hivyo
vya unyanyasaji wa kimwili. Tafiti nyingine zinaonyesha kwamba,
asilimia 30 ya wanawake hao hukabiliwa na mahusiano ya kijinsia ya
kulazimishwa. Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Afya Duniani WHO
ambalo pia linapambana na vitendo vya ukatili na unyanyasaji wa
kifamilia duniani, inaelezwa kuwa, ukatili wa mume dhidi ya mke na
unyanyasaji wa kijinsia, ni vitendo ambavyo vimeenea sana dhidi ya
wanawake duniani. Kwa mfano, ripoti iliyotolewa na shirika hilo
inaonyesha kwamba, kiwango cha unyanyasaji wa kifamilia nchini Ethiopia,
kimefikia asilimia 71. Wanawake wanaokumbwa na vitendo hivyo kwa muda
mrefu huathiriwa na matatizo ya mfadhaiko wa moyo, lishe duni na msongo
wa mawazo na matatizo mengineyo. Karibu asilimia 90 ya wahanga wa
vitendo vya unyanyasaji wa kifamilia huko nchini China pia wanatajwa
kuwa ni wanawake. Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na Shirikisho la
Wanawake nchini China CWF mwanamke mmoja kati ya watatu ni muathirika wa
ukatili wa kifamilia.
Magendo ya wanawake na utumwa wa kijinsia ni matatizo mengine ya
unyanyasaji dhidi ya wanawake, vitendo ambavyo vimeongezeka sana katika
nchi za Ulaya. Vitendo hivyo pia vimeshika kasi huko Marekani. Kwa
mujibu wa mtandao wa habari wa Lemondrop wa nchini Marekani, kila mwaka
karibu watu elfu 20 husafirishwa kwa magendo nchini humo kwa kisingizio
cha nafasi za kazi na masomo. Mbali na Marekani, vitendo vya magendo ya
utumwa wa wanawake na wasichana vimeenea sana nchini Uingereza na nchi
nyingi za Ulaya. Tukitoka Magharibi, nchi za Mashariki ya Kati ikiwemo
Saudi Arabia, Bahrain na Misri ni nchi ambazo zimeshamiri vitendo vya
unyanyasaji dhidi ya wanawake. Ni wazi kwamba, kutozingatiwa haki za
msingi za binadamu na za wanawake, ni sababu ya kuongezeka vitendo hivyo
katika nchi hizo. Hadi sasa wanawake wa Saudia bado wananyimwa haki zao
za kimsingi kabisa. Mfalme wa nchi hiyo amepitisha sheria ambayo
inawanyima wanawake haki za kimsingi kabisa ikiwemo ya kuendesha gari
huku wakitakiwa kufanya kazi nyingi za nje ya nyumba kwa idhini ya waume
zao. Kutokana na sheria kali za kuwazuia kuendesha magari, wanawake wa
Saudia hulazimika kwenda nchi nyingine kwa ajili ya kusomea udereva na
kupata leseni za kuendesha gari. Hii ni katika hali ambayo hivi karibuni
Baraza la Haki za Binaadamu la Umoja wa Mataifa lilipasisha mapendekezo
likiitaka nchi hiyo iboreshe hali ya haki za kibinaadamu nchini sanjari
na kuitaka ikomeshe ubaguzi na ukandamizaji dhidi ya wanawake.
Ukandamizaji unaotokana na vita ni miongoni mwa matatizo mengine
yanayowakabili wanawake duniani. Licha ya kwamba wanawake huwa hawana
nafasi yoyote katika mizozo ya silaha, lakini wao na watoto wadogo
wamekuwa wahanga wakubwa wa mizozo hiyo. Hivi sasa wanawake na mabinti
wengi wa Kiislamu huko Palestina, Gaza, Lebanon, Iraq, Syria,
Afghanistan na Pakistan, ni wahanga wakubwa wa ukandamizaji na ukatili
unaotokana na vita. Wanawake na watoto wa Myanmar pia hawajasalimika na
unyanyasaji na ukandamizaji huo. Wanawake na watoto wamekuwa wahanga
wakubwa wa mauaji ya umati yanayofanyika nchini humo dhidi ya jamii
ndogo ya Waislamu. Aidha huko Gaza na Palestina kwa ujumla, wanawake na
wasichana wamekuwa wahanga wakubwa wa mashambulizi ya utawala katili wa
Kizayuni, ambapo wengi wao wameuawa, kujeruhiwa, kufungwa jela na
kufanywa wakimbizi. Wakati hayo yakijiri, kwa upande mwingine
unyanyasaji wa kijinsia umeibuka katika nchi za Mashariki ya Kati
kufuatia jinamizi la vitendo vya uharibifu vya Uwahabi na makundi ya
kufurutu mipaka. Kwa masikitiko makubwa fatwa iliyotolewa na sheikh
mmoja wa Kiwahabi wa nchini Jordan aliyehalalisha kutekwa nyara na
kubakwa mabinti wa Kiislamu huko nchini Syria, imepelekea kuongezeka
jinai na ukatili dhidi ya wanawake wa nchi hiyo inayoshuhudia vita vya
ndani. Suala hilo limezidi kushika kasi kiasi kwamba hivi karibuni
shirika moja la nchini Misri lilitangaza wazi kuwashikilia mabinti wa
Syria kwa ajili ya kuwapelekea wanaume wapenda anasa na wazinifu
wanaodai kupigana jihadi huko Syria. Katika ripoti yake shirika hilo
lilitangaza kuwa, lina wasichana wavaa hijabu na niqab kutoka Syria kwa
kiwango kinachohitajika. Huu ni ukatili wa kijinsia wa hali ya juu na wa
wazi dhidi ya wanawake katika zama hizi. Inawezekana vipi katika karne
hii ya 21 kutangazwa wazi wazi unyanyasaji wa kuchupa mipaka wa aina
hiyo dhidi ya wanawake mbele ya kimya cha jamii ya kimataifa? Kama hiyo
haitoshi, kiongozi mmoja wa Kiwahabi amewataka wanawake kwenda nchini
Syria kwa ajili ya kuwaridhisha kijinsia wapiganaji wa kigaidi nchini
humo. Wasichana wengi walioathiriwa na fatwa hiyo kwa siku moja walikuwa
wakiingiliwa kingono na wanaume kadhaa tofauti ambapo baadhi yao
walifichua jinai hizo baada ya kurejea makwao kutoka Syria.
Wapenzi wasikilizaji, kipindi chetu cha makala ya wiki kinaishia hapa
kwa leo. Ni matumaini yangu kuwa mmenufaika vya kutosha na makala hii.
Mimi ni Sudi Jafar Shaban, msikose kuungana nami tena katika kipindi
kingine cha makala ya wiki katika siku na saa kama hii, hadi wakati
mwingine ninakuageni kwa kusema, kwaherini.
No comments:
Post a Comment