Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, December 18, 2013

Matokeo ya duru ya pili ya uchaguzi wa Mali

Matokeo ya duru ya pili ya uchaguzi wa Bunge nchini Mali yanaonesha kuwa chama tawala nchini humo kimeshinda uchaguzi huo. Chama cha Muungano kwa Ajili ya Taifa (RPM) kimejinyakulia viti vingi zaidi vya Bunge la taifa la nchi hiyo. Ripoti zinasema kuwa, chama cha RPM kimepata viti 60 kati ya viti 147 katika duru ya pili ya uchaguzi wa Bunge uliofanyika siku ya Jumapili. Imeelezwa kuwa, chama cha Muungano kwa Ajili ya Demokrasia ya Kitaifa ambacho ni muitifaki wa chama pia kimeshinda viti 50.
Kwa msingi huo, chama tawala cha Rais wa Mali pamoja na waitifaki wake vimepata jumla ya viti 110 vya Bunge. Chama cha URD cha Soumaila Cisse mgombea aliyeshindwa katika uchaguzi wa rais, kimepata viti 19 katika duru ya pili. Baraza la Katiba la Mali lenye jukumu la kutangaza matokeo ya uchaguzi wa Bunge siku kadhaa zilizopita lilitangaza ushindi wa wagombea 20 katika duru ya kwanza ya uchaguzi huo na kusema kuwa, kura zitapigwa tena ili kuwatafuta washindi wa viti 127 vilivyobakia.
Matokeo hayo yaliyotangazwa yatakuwa rasmi baada ya kupasishwa na Mahakama ya Katiba. Ripoti zinaeleza kuwa uchaguzi huo wa duru ya pili ulifanyika kwa utulivu bila matukio yoyote ya vurugu. Mashambulizi yaliyofanywa na makundi ya wapinzani siku moja kabla ya uchaguzi huo kwa kiasi fulani yaliwatia hofu watu na kuwazuia kwenda vituoni kupiga kura. Mlipuko wa bomu lililokuwa limetegwa katika gari kaskazini mwa Mali asubuhi siku moja kabla ya uchaguzi huo, uliharibu tu jengo la benki katika mji wa Kidal. Kwa msingi huo idadi ya wananchi walioshiriki katika duru ya pili ya uchaguzi wa Bunge wa Mali ilikuwa ndogo na kiwango cha ushiriki kilikuwa cha asilimia 38.62.
Kiongozi wa timu ya wasimamizi wa Umoja wa Ulaya katika uchaguzi wa Mali, Louis Michel amesema kuwa, uchaguzi huo kwa ujumla ulifanyika vizuri. Michel ameeleza kuwa, uchaguzi huo ulitimiza vigezo vya kimataifa vya uchaguzi wa kidomekrasia. Wasimamizi 3,300 na wasimamizi wakuu 200 walihudhuria katika maeneo 54 ya uchaguzi, wakati wa zoezi la kupiga kura nchini Mali.

No comments: