Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, December 16, 2013

Tunao uwezo wa kukomesha umaskini duniani (kwa mnasaba wa Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Umaskini)

Karibuni wapenzi wasikilizaji katika makala hii maalumu tuliyokuandalieni kwa mnasaba wa Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Umaskini. Ni matumaini yetu mtakuwa nasi hadi mwisho wa kipindi.
Tarehe 17 Oktoba ambayo mwaka huu imesadifiana na siku ya Alkhamisi, huadhimishwa kila mwaka kwa jina la Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Umaskini.
Umoja wa Mataifa ndio uliotangaza siku hiyo kwa lengo la kuzijumuisha pamoja nguvu za mataifa yote ya dunia katika jambo moja, nalo ni kupambana na umaskini. Kila mwaka siku hiyo hutumiwa kutangaza mshikamano wa mataifa yote ya dunia kwa ajili ya kuwaliwaza na kuwasaidia wahanga wa ukata na majanga ya njaa na vile vile kutafuta njia za kuweza kung'oa kikamilifu mizizi ya umaskini na ubaguzi na kuleta heshima na utukufu wa mwanadamu.
Msingi wa kutengwa tarehe 17 Oktoba kuwa Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Umaskini umeanzia tangu mwaka 1987. Mwaka huo mamia ya maelfu ya watu walikusanyika mjini Paris Ufaransa kwa ajili ya kuadhimisha siku ya kupitishwa Hati ya Haki za Binaadamu ya Umoja wa Mataifa mwaka 1948. Watu waliokusanyika mjini Paris walipitisha kwa kauli moja kuwa umaskini ni aina fulani ya uvunjaji wa haki za binadamu na kwamba haiyumkiniki kulindwa haki za binadamu madhali umaskini ungalipo duniani. Tangu mwaka huo, taasisi nyingi duniani zilianza kuendesha kampeni ya kuwaelimisha na kuwaamsha walimwengu kuhusu majakamoyo ya umaskini na ilipofika tarehe 17 Oktoba mwaka huo, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa likaitangaza rasmi siku hiyo kuwa ni Siku ya Kimataifa ya Kupambana na Umaskini. Suala la kupambana na umaskini lilipata nguvu sana kuanzia mwaka 2000 wakati ilipopasishwa Hati ya Milenia ambayo moja ya malengo yake makuu lilikuwa ni kuhakikisha umaskini umepungua kwa kiwango kikubwa duniani ifikapo mwaka 2015. Ni vyema kusema hapa kwamba, licha ya kuweko jitihada mbalimbali za kufanikisha malengo ya milenia ya kukata mizizi ya umaskini duniani, lakini hadi hivi sasa asilimia 20 ya walimwengu wanaishi kwenye umaskini mutlaki. Umoja wa Mataifa unaendesha miradi mbalimbali ya kufanikisha malengo ya milenia yanayotakiwa kufikiwa ifikapo mwaka 2015 ukiwa na matumiani kwamba ifikapo mwaka huo, utakuwa umefanikiwa kupungaza umaskini kwa kiwango kikubwa duniani. Hata hivyo kutokana na kushindwa kufikiwa malengo hayo, hivi sasa Umoja wa Ulaya umekuja na fikra nyingine ya kupunguza umaskini katika muongo ujao. Tab'an kuna mafanikio ya kiasi fulani yamepatikana katika jitihada za kupambana na umaskini. Hilo linathibitishwa na Mkuu wa Benki ya Dunia aliposema: "Sisi katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, tumeshuhudia harakati za kihistoria ambazo zimepelekea kupungua idadi ya watu wanaoishi kwenye umaskini, lakini bado kuna watoto wadogo duniani ambao wanaishi katika ukata wa kupindukia ambao bila ya shaka yoyote hakuna kazi iliyofanyika kwa ajili yao." Mwisho wa kunukuu.
 

Bila ya shaka yoyote neno umaskini ni maarufu na kila mmoja analijua neno hilo. Lakini ni nini maana ya watu maskini? Inaposemwa watu hawa ni maskini kwa mujibu wa maana iliyotolewa kimataifa ni kwamba hao ni watu, au kaya, au familia, au kundi la watu ambao vyanzo vyao vya kiutamaduni, kimaada na kijamii ni vichache kiasi kwamba wanashindwa kufaidika na suhula za chini kabisa katika maisha yao jambo ambalo linawapambanua na watu wengine wanaoishi nao katika jamii. Ili kutoa ufafanuzi zaidi, Umoja wa Mataifa umetoa maana jumla ukisema kuwa, nchi zenye pato la wastani na la juu inabidi familia za watu wa nchi hiyo wanaoishi kwa pato la chini ya asilimia 50 hadi asilimia 60 ya wastani wa pato la nchi wahisabiwe kuwa ni watu maskini. Amma kwa upande wa nchi zenye pato dogo zaidi, watu wanaoishi kwa kipato cha chini ya dola 1.25 kwa siku wanahesabiwa kuwa ni maskini. Licha ya kwamba kumefanyika jitihada mbalimbali za kupambana na umaskini, lakini hadi hivi sasa bado asilimia 20 ya watu duniani wanaishi kwa pato la chini ya kiwango hicho tulichokitaja, hivyo wanahesabiwa kuwa wanaishi chini ya mstari wa umaskini. Hii ni katika hali ambayo karibu watoto milioni 7 wa chini ya umri wa miaka mitano wanasumbuliwa na lishe duni. Kwa mujibu wa malengo mapya ya Benki ya Dunia, inabidi ifikapo mwaka 2030 idadi ya watu maskini duniani ipungue kwa asilimia tatu.  Jim Yong Kim, Mkuu wa Benki ya Dunia amesema kuwa, nchi 188 duniani ambazo ni wanachama wa taasisi hiyo ya kimataifa ya fedha zinapaswa kufanya jitihada zao zote na kuongeza kasi katika juhudi zao za kuangamiza umaskini. Amesema, kuna wajibu kwa nchi hizo kushirikiana vilivyo kuhakikisha kuwa malengo ya mwaka 2030 ya benki hiyo yanafikiwa. Aidha amesema, kupambana na ukata na kuleta ustawi kwa vizazi vijavyo ni miongoni mwa malengo makuu ya Benki ya Dunia.
Kiujumla ni kuwa, umaskini ni miongoni mwa mambo tata sana yanayomsumbua mwanadamu. Sababu yake ni kuwa, sababu zinazopelekea kutokea umaskini ni nyingi sana. Hazihusiani na makosa ya kibinadamu tu, bali umaskini unachangiwa pia na masuala ya kimaumbile kama vile ukame, ukosefu wa mvua, maradhi katika mimea, nzige n.k. Sababu nyingine ni wanadamu wenyewe. Madhalimu wanawanyonya wanyonge na kujilimbikizia utajiri peke yao huku walimwengu wakiteseka kwa umaskini. Umaskini nao si kitu cha kupita na wala si kitu cha muda mfupi, bali ni kitu ambacho vizazi kwa vizazi vya wanadamu vinarithishana umaskini. Wataalamu wanasema kuwa, ni vigumu kumaliza ukata na umaskini duniani ila kwa kuwekeza kwenye watoto wadogo kwa ajili ya vizazi vijavyo. Wanasema inabidi uweko uadilifu katika upatikanaji na utumiaji wa suhula mbalimbali muhimu kama vile elimu bora, huduma za afya, uwekezaji, usalama, kujenga misingi madhubuti ya kifamilia n.k. Hivyo tunathubutu kusema kuwa, watu wanaoteseka kwa umaskini hivi sasa, wanahitajia zaidi misaada ya kweli ya kivitendo kulikoni maneno ya kuwaliwaza tu.
Ukitoa njia tuliyotangulia kusema ya kuwekeza katika watoto wadogo, kuna njia nyingine nyingi za kuweza kuumaliza kabisa umaskini duniani. Kuna haja ya kufanyika jitihada za kweli za kutoka kwenye umaskini kuelekea kwenye ustawi na maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kiutamadunia katika nchi zilizobaki nyuma kimaendeleo. Jamii yeyote ambayo uchumi wake haukuwi, kwa kweli uwezo wake wa kujiletea maendeleo ya kiuchumi ni mdogo na haiwezi kunyanyua kiwango cha ustawi wa watu yake. Uzoefu unaonesha kuwa, silaha bora kabisa ya kupambana na adui umaskini ni kuandaa fursa za kazi kupitia kuongeza uwekezaji katika sekta za viwanda na kilimo, sambamba na kuanzisha maeneo ya uzalishaji bora na kushirikishwa vilivyo mataifa ya dunia katika mabadilishano ya kimataifa. Juhudi za kuleta uadilifu wa kijamii na kugawanywa kiuadilifu utajiri kati ya matabaka mbalimbali ya watu kwenye jamii, nazo zina umuhimu mkubwa sana katika kupunguza na hatimaye kumaliza kabisa umaskini duniani. Hata hivyo, siasa za kikoloni za nchi zinazopenda makuu nazo zinachangia pakubwa katika kufukarika na kuwa maskini kupindukia mataifa mengine. Ni jambo lililo wazi kuwa madola ya kibeberu ndiyo kikwazo kikuu kinachokwamisha juhudi za kupambana na umaskini duniani. Bila ya shaka yoyote iwapo nchi za kibeberu zitaachana na siasa zao za kutenga fedha nyingi kugharamia masuala ya kijeshi, zitasaidia sana katika kumaliza umaskini ulimwenguni. Ni jambo lisilo na shaka pia kwamba, kusamehewa madeni yao nchi maskini na kuandaliwa uwanja wa kuweza nchi hizo kufaidika na teknolojia za kisasa, nayo ni njia nyingine inayoweza kuondoa umaskini ulimwenguni. Ni kwa sababu hii ndio maana kichwa cha maneno cha makala yetu hii kikawa: Tunao uwezo wa kukomesha umaskini duniani. Naam, kama kutakuwepo siasa sahihi, na iwapo mataifa ya dunia yataheshimu makubaliano ya kimataifa na endapo litapigwa vita kikamilifu suala la kutumiwa fedha nyingi katika masuala ya kijeshi na kuingilia mambo ya ndani ya mataifa mengine kwa ajili ya kuyakoloni, basi bila ya shaka yoyote jakamoyo la ukata na umaskini linaweza kuondoka kikamilifu duniani.

No comments: