Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, December 28, 2013

Miripuko ya mabomu Beirut nchini Lebanon

Kwa mara nyingine tena jana Ijumaa, wananchi wa Beirut mji mkuu wa Lebanon walishuhudia mripuko mkubwa wa bomu uliosababisha vifo vya watu wasiopungua wanane akiwemo Muhammad Shatar, waziri wa zamani wa fedha katika serikali ya Fouad Siniora na makumi ya wengine kujeruhiwa. Lebanon ambayo kipindi fulani ilijulikana kama ardhi nyeupe katika eneo la Mashariki ya Kati, hivi sasa inakabiliwa na hali ya ukosefu wa amani na utulivu na inalengwa na mashambulizi ya miripuko ya mabomu yanayoua na kujeruhi mamia ya watu wasio na hatia.
Miongoni mwa watu waliouawa kwenye miripuko mbalimbali iliyotokea nchini humo, wako shakhsia wa kisiasa na kijeshi, kama Hassan al Lakkis, kamanda wa ngazi za juu wa Hizbullah ya Lebanon na Sheikh Ibrahim Ansari aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Utamaduni cha ubalozi wa Iran mjini Bairut.
Lebanon iko tofauti kabisa na nchi nyingi za Kiarabu, kwani nchi hiyo haitawaliwi kidikteta na wala haikabiliwi na malalamiko ya mara kwa mara ya wananchi dhidi ya serikali.  Mzunguko katika muundo wa kisiasa na kiuongozi uko wazi kabisa nchini humo. Wananchi wa Lebanon si wageni hata kidogo katika masuala ya uchaguzi na hata ushiriki wao katika uwanja wa kisiasa. Tunaweza kusema kuwa, Lebanon kwa miaka kadhaa sasa inaonekana kuwa mstari wa mbele katika kupiga hatua za kisiasa na kuimarisha muundo wa taasisi za kiraia, ikilinganishwa na nchi nyingine za Kiarabu na hasa zile zenye ushawishi mkubwa katika eneo la Mashariki ya Kati.
Alaa kulli haal, sababu kuu ya kukosekana amani na utulivu nchini Lebanon inatokana na hitilafu za kisiasa na hujuma za makusudi zinazofanywa na makundi ya kisiasa na hasa mrengo wa al Mustaqbal kuhusiana na suala la kuundwa serikali ya umoja wa kitaifa, hujuma ambazo bila shaka zina maslahi kwa baadhi ya nchi za Kiarabu na utawala wa Kizayuni wa Israel. Hakuna shaka kuwa, mivutano ya kisiasa na kutoundwa serikali ya Tammam Salam Waziri Mkuu mteule, ni moja kati ya sababu kuu za kuongeza machafuko katika maeneo mbalimbali nchini Lebanon.
Waokoaji wakifuatilia tukio hilo.

Suala jingine ambalo hatupaswi kulipuuza ni hili kwamba, hivi sasa Lebanon inaathiriwa mno na machafuko yanayoendelea nchini Syria. Serikali ya Lebanon ni miongoni mwa nchi chache ambazo tokea yalipoanza machafuko nchini Syria, daima imekuwa mstari wa mbele kupinga uingiliaji wa madola ya kigeni kwenye mgogoro wa nchi hiyo. Wakati mipaka ya nchi kama Jordan na Uturuki imekuwa wazi na inatumiwa kupitisha silaha zinazopelekwa kwa makundi ya kigaidi yanayopigana na serikali ya Rais Bashar Assad, Lebanon haikutoa fursa hata kidogo ya kutumiwa mipaka yake kwa lengo la kuwapelekea silaha magaidi na mamluki wa nchi za Magharibi na za Kiarabu huko Syria. Hali kadhaika, hatua ya Hizbullah ya kulisaidia jeshi la Syria baada ya utawala wa Israel kushambulia vituo vya kiutafiti, iliongeza nguvu za kijeshi za Syria katika kukabiliana na makundi ya kigaidi, jambo ambalo lilizichukiza nchi za Magharibi na vibaraka wao wa Kiarabu na huenda suala hili ndiyo sababu ya kuongezeka operesheni za kigaidi ndani ya ardhi ya Lebanon. Baadhi ya makundi ya kigaidi ya Syria yaliwapeleka wanamgambo wao ndani ya ardhi ya Lebanon ili kutekeleza operesheni za kigaidi nchini humo. Makundi mengine yanayofungamana na mitandao ya kigaidi yanafanya juhudi za kuweka kambi zao ndani ya ardhi ya Lebanon.
Imeelezwa kuwa, lengo la kuwepo magaidi ndani ya ardhi ya Lebanon ni kutoa pigo kwa Hizbullah na kuzidisha operesheni za kigaidi dhidi ya shakhsia wa kisiasa na kijeshi wa Lebanon ili jeshi la nchi hiyo lielekeze nguvu zake zaidi ndani katika kukabiliana na makundi ya kigaidi na kuacha kushughulikia maeneo ya mipakani, ili makundi hayo ya kigaidi yapate mwanya wa kupitisha silaha zao na kuzipeleka Syria.
Nukta muhimu nyingine ya kuzingatiwa ni  kwamba, Sirajuddin Zuraiqat kiongozi wa kundi la kigaidi linalowakufurisha Waislamu, siku ya Alhamisi iliyopita alitoa mkanda wa video na kutishia kwamba, Beirut itashuhudia miripuko mipya ya kigaidi hivi karibuni.
Ni kwa kuzingatia ushahidi huo, ndipo tukamuona Adnan Mansour Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Lebanon katika radiamali yake aliyoitoa mara baada ya mripuko huo wa jana akasema kuwa, mripuko huo ni katika taathira za mgogoro wa Syria. Naye Shakib Qortbawi Waziri wa Sheria wa Lebanon amesema kuwa, mripuko huo umeongozwa kutoka nje ya nchi hiyo.

No comments: