Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, December 18, 2013

Kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu Syria

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa mara nyingine tena limeitisha kikao na kujadili kadhia ya Syria. Kikao hicho cha faragha cha Baraza la Usalama kilifanyika jana huku mada mbili kuu zikitawala mkutano huo. Maudhui ya kwanza iliyojadiliwa katika mkutano huo ni silaha za kemikali zilizotumika Syria na mkutano wa Geneva-2. Nukta muhimu katika kikao hicho ni kwamba, mwakilishi wa Russia katika Umoja wa Mataifa alizikosoa vikali siasa na misimamo ya Marekani kuhusiana na mgogoro wa Syria. Vitaly Ivanovich Churkin, ameituhumu Marekani kwamba, imepuuza takwa la Russia la kuitaka Washington itoe nyaraka na ushahidi wa kuonesha kwamba, serikali ya Syria ilitumia silaha za kemikali dhidi ya raia. Amesema, madai ya Marekani kwamba, serikali ya Syria ilihusika na shambulio hilo hayakinaishi na kwamba, Moscow inaamini kwamba, shambulio hilo la kichochezi lilifanywa na wanamgambo wanaobeba silaha nchini Syria. Mwakilishi wa Russia katika Umoja wa Mataifa amesema kwamba, Moscow ina ushahidi unaoonesha kwamba, kuanzia Disemba mwaka 2012, serikali ya Marekani ilikuwa na taarifa kuwa, muda si mrefu mashambulizi ya silaha za kemikali yatafanyika nchini Syria. Swali la kimsingi ni kwamba, kwa nini Washington ilinyamaza kimya licha ya kuwa na taarifa kuhusiana na jambo hilo? Baadhi ya duru zinapinga madai ya Marekani kwamba, serikali ya Syria ndiyo iliyohusika na shambulio la silaha za kemikali za gesi ya Sarin. 
 
Kuuawa wanajeshi wa serikali na raia katika mashambulio tofauti ya kemikali nchini Syria na ushirikiano mkubwa uliooneshwa na serikali ya Rais Bashar al-Assad kwa wakaguzi wa Umoja wa Mataifa sambamba na kukubaliana serikali hiyo na suala la kuangamizwa silaha hizo ni ushahidi tosha kwamba, serikali ya Damascus haikuhusika na shambulio hilo. Katika upande wa pili, kwa kuzingatia kwamba, daima wanamgambo wanaobeba silaha nchini Syria wamekuwa wakitafuta kisingizio ili Syria ivamiwe kijeshi na madola ya kigeni, dhana ya kwamba, waasi hao ndio waliohusika na shambulio la kemikali inazidi kupata nguvu. Hasa kwa kutilia maanani kwamba, ushahidi unaonesha kuwa, hakuna jinai nchini Syria ambayo haijafanywa na magaidi na waasi hao. Duru za kitiba nchini Syria zimetangaza kwamba, raia 80 wameuawa kwa umati na magaidi hao katika eneo la Rif Dimashq. Je makundi ya kitakfiri yanaofanya jinai kama hizo hayawezi kutumia silaha za kemikali dhidi ya raia na askari wa serikali? Nukta ya kutaamali zaidi ni kwamba, jinai kama hizo zimekuwa zikifanyika kwa baraka na idhini ya Marekani. Serikali ya Marekani ni miongoni mwa waungaji mkono wakuu wa magaidi wa Syria katika kipindi cha miaka hii mitatu ya mgogoro huo. Hivi sasa pia ambapo kuna juhudi za kuhakikisha kunafanyika mkutano wa Geneva-2 kwa shabaha ya kuupatia ufumbuzi wa kisiasa mgogoro wa Syria, Marekani ndio kwanza wanaendelea kuzungumzia udharura wa kuungwa mkono makundi ya kigaidi nchini Syria.

No comments: