Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, December 16, 2013

Kujengwa majengo na bustani mahala ilipobomolewa misikiti nchini Bahrain

Utawala wa Aal Khalifa nchini Bahrain unafuta alama za Kiislamu kwa kujenga majengo na bustani za kupumzikia mahala ulipobomoa misikiti katika harakati za mapinduzi ya wananchi nchini humo. Mtandao wa mrengo wa upinzani wa Februari 14, umewanukuu wakazi wa kijiji cha Aali wakisema kuwa, utawala wa Aal Khalifa unajenga jengo katika eneo kulipobomolewa na askari wa utawala huo, msikiti wa Amir al-Barghuthi.
Hii ni katika hali ambayo licha ya kubomolewa msikiti huo, wakazi wa kijiji hicho bado wanasali katika eneo hilo. Viongozi na shakhsia wa kidini nchini Bahrain wamesisitiza kwa mara kadhaa kuwa, hakuna mtu mwenye haki ya kuhodhi na kutumia hata dhiraa ya ardhi ya kidini hata kama ni mahala ilipobomolewa misikiti na askari wa utawala wa kidikteta wa nchi hiyo. Mashirika mbalimbali ya Kimataifa na lile la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kwa pamoja yamelalamikia hatua ya utawala wa Aal Khalifa ya kubomoa misikiti ya kale nchini humo. Kabla ya hapo Baraza la Kiislamu na kituo cha watetezi wa haki za binaadamu nchini humo yalikuwa yametangaza kuwa, mkuu wa kongresi ya kijamii ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) anazo taarifa kuhusiana na jinai za utawala wa Aal Khalifa za kubomoa msikiti wa kihistoria wa al-Berighi uliojengwa mnamo mwaka 1549 yaani miaka 464 iliyopita. Katika ripoti iliyowasilishwa kwenye ofisi ya UNESCO, Sheikh Maitham al-Selman kiongozi wa kitengo kinachohusika na uhuru wa kuabudu katika kituo cha watetezi wa haki za binaadamu nchini Bahrain ameeleza kuwa jumla ya misikiti 38 imebomolewa na utawala wa nchi hiyo.

Kabla ya hapo pia na licha ya kuwepo upinzani mkubwa wa wananchi, utawala huo ulikuwa umeanza shughuli za ujenzi wa bustani ya kupumzikia katika eneo la msikiti wa Abudharri. Msikiti huo ulibomolewa na askari watiifu kwa utawala wa kifalme wa Aal Khalifa miaka miwili iliyopita baada ya kutangazwa kwa hali ya hatari nchini Bahrain. Kuhusiana na hali hiyo Jumuiya ya Kitaifa ya al Wifaq imetoa ripoti ya kulaani ubomoaji misikiti nchini humo na kusema, mashambulizi dhidi ya Husseiniya na kubomolewa majengo hayo ya kidini ni miongoni mwa jinai za utawala wa Aal Khalifa ambazo zimekuwa zikitekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu ya hivi karibuni dhidi ya matukufu ya kidini. Sheikh Ali Salman amesema kuwa, katika kipindi cha vuguvugu la mapinduzi ya Bahrain wananchi hawajawahi kufanya shambulizi lolote dhidi ya msikiti. Hii ni katika hali ambayo utawala wa kifalme wa ukoo wa Aal Khalifa umeshabomoa makumi ya misikiti na Husseiniya ikiwemo pia misitiki ya kihistoria. Kwa upande mwingine Sheikh Maitham al-Selman ambaye pia ni mjumbe wa kituo cha haki za binaadamu nchini Bahrain, ametaka kuundwe tume huru ya kimataifa ya uchunguzi ili kukomesha mara moja mashambulizi dhidi ya maeneo ya ibada katika maeneo tofauti ya Bahrain. Aidha kiongozi huyo ametaka kukomeshwa uchochezi wa kikaumu na kimadhehebu unaofanywa kupitia vyombo vya habari mbalimbali nchini Bahrain. Tangu mwaka 2011 lilipoanza vuguvugu la mapinduzi ya wananchi wa Bahrain utawala wa kidikteta wa Aal Khalifa umebomoa makumi ya misikiti ya Waislamu wa Kishia katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo na kukataa kuijenga tena misikiti hiyo katika maeneo hayo.

No comments: