Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, December 16, 2013

Kuanzishwa chama kipya cha upinzani nchini Uganda

Jenerali David Sejusa, mkuu wa zamani wa vyombo vya kiintelijensia nchini Uganda ametangaza kuwa, ameanzisha chama kipya cha kisiasa cha upinzani. Jenerali huyo mstaafu aliyekimbilia nchini Uingereza, amewaambia waandishi wa habari mjini London kwamba, anapanga kugombea kiti cha Urais katika uchaguzi ujao kwa tiketi ya chama chake cha The Freedom and Unity Front.  Weledi wa mambo wanaamini kwamba, kuundwa chama kipya cha kisiasa nchini Uganda hakuna maana si jaribio la kumuondoa Rais Museveni katika ulingo wa kisiasa, bali ni hatua moja mbele ya kutaka kumuweka kando mtoto wa Rais Museveni ambaye anataka kuwania kiti cha Urais nchini Uganda katika uchaguzi ujao uliopangwa kufanyika mwaka 2016.
Hii ni katika hali ambayo, mwana wa Rais Museveni, Brigedia Muhoozi Kainerugaba hadi sasa hajakanusha tetesi za kutaka kugombea kiti cha Urais katika uchaguzi ujao nchini Uganda. Weledi wa mambo ya kisiasa wanaamini kuwa, kupandishwa vyeo haraka haraka jeshini mwana huyo wa Museveni kunaashiria kuwa anaandaliwa kumrithi baba yake. Hasa kwa kutilia maanani kwamba, washauri wa Rais Museveni hawaoni kama Museveni ana hamu ya kugombea tena Urais kwa mara ya tano mfululizo. Wapinzani nchini Uganda wanalalamika kuwa, kipindi cha karibu miaka 28 cha utawala wa Rais Museveni kimeambatana na kukandamizwa vibaya wapinzani pamoja na wakosoaji wa serikali yake. Wapinzani hao wanatoa mfano wa kufutwa kazi Erias Lukwago, aliyekuwa meya wa Kampala wakisema kuwa huo ni ushahidi tosha wa kuthibitisha madai yao hayo. Daktari Kizza Besigye kiongozi  wa zamani wa FDC na mpinzani mkuu wa Museveni ameshindwa mara tatu katika kinyang'anyiro cha Urais.

Katika uchaguzi uliopita uliofanyika mwaka 2011, Rais Museveni alipata asilimia 68 ya kura na kumshinda kwa mara nyingine tena hasimu wake wa kisiasa Kizza Besigye aliyepata asilimia 26 ya kura. Pamoja na hayo waangalizi wa uchaguzi huo kutoka Umoja wa Ulaya walitangaza kuwa, hatua ya serikali ya Uganda ya kusambaza askari  katika barabara za Kampala na katika miji mikubwa ya nchi hiyo ya Afrika Mashariki ililenga kuzusha woga na wasi wasi baina ya wananchi katika siku ya kupiga kura. Wakosoaji wa serikali ya Uganda wanaamini kwamba, kukandamizwa wapinzani na wanaharakati wa kisiasa wa Uganda ndio udhaifu mkubwa wa serikali ya Rais Museveni. Baada ya Rais Museveni kuingia madarakani mwaka 1986, alipiga marufuku shughuli za vyama vya kisiasa. Hata hivyo mashinikizo ya kieneo na kimataifa yalimuelemea na ndio maana mwaka 2005 alilazimika kufungua mlango vyama vya kisiasa na kuviruhusu kuendesha shughuli zao. Hivi sasa kuna vyama vingi vya kisiasa nchini Uganda lakini havina nguvu za kushindana na chama tawala cha NRM katika uchaguzi. Baadhi ya wachambuzi wa mambo wanasema kuwa, kuanzishwa chama kipya cha kisiasa na Jenerali David Sejusa mkuu wa zamani wa vyombo vya kiintelejensia nchini Uganda kunaweza kutathminiwa kuwa ni changamoto nyingine kubwa kwa chama tawala katika uchaguzi ujao.

No comments: