Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, December 25, 2013

Jinai za utawala wa Kizayuni katika mwaka wa 2013 dhidi ya Wapalestina

Huku mwaka wa 2013 ukiwa umefikia katika siku zake za mwisho, Ofisi ya Masuala ya Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa imetangaza kuwa, mwaka 2013 utawala wa Kizayuni wa Israel umewafanyia ukatili mara 300 Wapalestina. Taarifa ya ofisi hiyo ya Umoja wa Mataifa inayohusiana na jinai na ukatili wa wanajeshi na walowezi wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina imeongeza kuwa, katika mwaka 2013 wanajeshi wa Israel wameshambulia maeneo mbalimbali ya Palestina na kuua makumi ya Wapalestina na kuwajeruhiwa wengine 3,753.
Fauka ya hayo, walowezi wa Kizayuni nao wamengoa zaidi ya miti elfu 10 ya mizaituni ya Wapalestina katika muda huo kitendo ambacho takwimu zinaonesha kuwa kimeongezeka mara 25 ikilinganishwa na mwaka uliopita yaani 2012. Kabla ya hapo pia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha kwa wingi wa kura haki ya Wapalestina ya kumiliki ardhi zote zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni tangu mwaka 1967 ukiwemo mji mtakatifu wa Baytul Muqaddas, jambo aambalo ni tangazo jengine la jamii ya kimataifa kwamba inapinga ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni katika ardhi za Wapalestina. Hii ni katika hali ambayo, mazungumzo ya mapatano kati ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina na utawala wa Kizayuni wa Israel yaliyokuwa yamekwama kwa muda wa miaka mitatu yalianza tena mwezi Julai mwaka huu kwa mashinikizo ya Marekani kwa Wapalestina na kuendelea hadi siku chache zilizopita.

 Weledi wa mambo wanaamini kuwa viongozi wa utawala wa Kizayuni katika kipindi chote hiki cha mazungumzo yanayokwama na kukwamuka kati ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina na Wazayuni, viongozi wa Israel siku zote wamekuwa wakipoteza muda tu, hawajawahi kuheshimu hata mara moja mazungumzo hayo na daima wamekuwa wakiendeleza siasa zao za wizi na kupora mali za Wapalestina. Kwa maneno mengine ni kuwa, serikali mbalimbali za utawala wa Kizayuni katika kipindi chote hiki cha miaka 20 ya mazungumzo na Wapalestina, zimekuwa zikijionesha kwamba zinapenda amani, lakini kila leo Wazayuni wanafanya jinai dhidi ya Wapalestina, wanapora ardhi zao, wanavunja makazi yao, wanaharibu mashamba yao na wanawashambulia kikatili kwa kila aina ya silaha, huku wakiwazingira kila upande Wapalestina hao madhlumu. Saib Uraiqat, mkuu wa timu ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina inayofanya mazungumzo ya mapatano na Wazayuni amesema kuwa, mazungumzo ya moja kwa moja ya mapatano kati ya mamlaka hiyo na Wazayuni kwa upatanishi wa Marekani yamekwama muda mrefu nyuma na kwamba kinachofanyika hivi sasa ni mazungumzo kati ya Wapalestina na Wamarekani kwa upande mmoja, na Wamarekani na Wazayuni kwa upande wa pili. Jambo hilo nalo lina maana ya kwamba siasa za miaka 20 sasa za Mamlaka ya Ndani ya Palestina za kufanya mazungumzo na Wazayuni zimefeli kikamilifu na zimekuwa ni kwa madhara ya Wapalestina. Ni kwa sababu hiyo ndio maana wachambuzi wa mambo wakasema kuwa, msimamo wa makundi ya muqawama ya Palestina kwamba utawala wa Kizayuni hauelewi lugha yoyote isipokuwa mtutu wa bunduki, ndio uliowaletea manufaa Wapalestina na si siasa za kukubali kuburuzwa kwenye mazungumzo yenye madhara makubwa kwa taifa la Palestina zinazoendeshwa na Mamlaka ya Ndani ya Palestina.

No comments: