Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Thursday, July 18, 2013

Ubaguzi wa rangi wazusha mjadala Italia

Naibu Spika wa Baraza la Seneti la Italia Roberto Calderoli ambaye amemfananisha Waziri wa Uhamiaji wa nchi hiyo mwenye asili ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Cecile Kyenge kuwa ni "orangutangu" kwa maana ya nyani mkubwa wa mwituni, amesema kuwa, hatajiuzulu kwa sababu ya matamshi hayo.
Naibu Spika wa Baraza la Seneti la Italia amesema licha ya kwamba ameomba radhi kutokana na matamshi hayo, lakini wanachama wengi wa chama chake cha Northern League hawataki ajiuzulu.

Dharau na matamshi hayo ya kejeli na utovu wa adabu ya seneta wa Italia dhidi ya waziri mwenye asili ya Afrika wa nchi hiyo yamezua wimbi kubwa la ukosoaji dhidi yake katika duru za habari na mitandao ya kijamii. Vyama na viongozi wa kisiasa wa Italia pia wanamshinikiza seneta Roberto Calderoli ajiuluzu.
Waziri Mkuu wa Italia Enrico Letta ameyataja matamshi hayo ya dharau ya Naibu Spika wa Baraza la Seneti la nchi hiyo dhidi ya waziri wa serikali yake kuwa ni doa jeusi katika historia ya Italia.
Cecile Kyenge ni mmoja kati ya waziri saba wa kike katika baraza la mawaziri la serikali Letta na amekuwa akisumbuliwa kwa hujuma za kibaguzi tangu alipochaguliwa kuchukua nafasi hiyo. Wapinzani wake hususan vyama vyenye misimamo mikali vya mrengo wa kulia, wamekuwa wakimtaka aondoke katika baraza la mawaziri la Italia. Hata hivyo Bi Kyenge amekuwa akisisitiza kuwa, anaona fakhari kuwa Mwafrika mweusi.
Cecile Kyenge ambaye alichaguliwa kuwa Waziri wa Uhamiaji wa Italia Aprili mwaka huu, amekuwa akifanya jitihada kubwa za koboresha hali ya wahajiri na wahamiaji nchini humo. Waziri huyo Mwafrika ana lengo la kuwasilisha muswada ambao utawatambua watoto wa wahamiaji wanaoishi nchini Italia kuwa ni raia wa nchi hiyo. Kwa mujibu wa sheria za sasa watoto wa wahajiri wa kigeni wanaozaliwa nchini Italia hawahesabiwi kuwa raia wa nchi hiyo na wanaweza kuomba uraia baada ya kukamilisha miaka 18. Kwa sababu hivyo vyama vyenye misimamo mikali ya kibaguzi vya mrengo wa kulia hususan kile kinachopiga vita wahajiri cha Northern League, vinapinga vikali sera za waziri Kyenge.
Seneta Calderoli ambaye ni kiongozi wa chama hicho cha Northern League, anasema sera za Waziri Cecile Kyenge zinawahamasisha wahajiri haramu kuingia nchini Italia.
Italia ni moja kati ya nchi zinazokusudiwa na wahajiri wa Kiafrika na inatumiwa na wahajiri hao kama lango la kuingilia katika nchi nyingine za Ulaya. Wahajiri hao hufanya kazi dunia na kwa ujira wa chini katika nchi nyingi za Ulaya.
Wachambuzi wa mambo wanasema kuwa matamshi ya Seneta Calderoli ambaye aliwahi kuwa waziri katika serikeli ya waziri mkuu aliyepita Silvio Berlusconi, yatawachochea Wataliano wenye misimamo mikali ya kibaguzi na kuzidisha mashambulizi ya kinyama dhidi ya wageni nchini Italia. Hususan ikizingatiwa kwamba kwa sasa Italia inasumbuliwa na matatizo makubwa ya kiuchumi. Deni la nchi hiyo pia limefikia yuro trilioni 3 na kiwango cha watu wasio na ajira kimeongezeka na kufikia asilimia 26.

No comments: