Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Thursday, July 18, 2013

Safari ya Kerry Mashariki ya Kati

John Kerry Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani Jumanne usiku alikutana na kufanya mazungumzo na Mahmoud Abbas Rais wa Serikali ya Ndani ya Palestina huko Jordan kwa shabaha ya kuhuisha eti mazungumzo ya amani Mashariki ya Kati. Mazungumzo hayo yamepingwa vikali na wananchi wengi wa Palestina. Akiwa katika safari yake ya sita katika eneo la Mashariki ya Kati baada ya kuteuliwa kuwa Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani, John Kerry
amefanya mazungumzo na Rais Mahmoud Abbas Rais wa Serikali ya Ndani ya Palestina katika juhudi za kuurejesha utawala wa Kizayuni na Wapalestina katika meza ya mazungumzo ya mapatano eti ya Mashariki ya Kati.
Japokuwa hakuna taarifa iliyotolewa kuhusu mazungumzo hayo yaliyofanyika kwa muda wa masaa matano, lakini nukta hii inapasa kutiliwa maanani kwamba, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani amelifanya suala la kufuatilia mchakato eti wa mapatano wa Mashariki ya Kati kuwa moja ya vipaumbele vyake vikuu katika ajenda yake tangu alipoteuliwa katika nafasi hiyo tarehe Mosi Februari mwaka huu.
Baada ya mazungumzo hayo ya Kerry na Abbas huko Amman nchini Jordan, imetangazwa kuwa Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani jana pia alitarajiwa kufanya mazungumzo na viongozi wa nchi zilizounga mkono mpango wa amani wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu wa mwaka 2002. Mpango huo unajumuisha kutambuliwa kikamilifu Israel iwapo majeshi ya utawala huo yataondoka katika ardhi za Palestina zilizoghusubiwa mwaka 1967 na kukubali kutatuliwa kwa uadilifu kadhia ya wakimbizi wa Kipalestina.
Mpango huo wa Arab League ambao umepingwa na  Israel, unakabiliwa na vizuizi vingi kwa kuzingatia kwamba, utawala wa Kizayuni si tu kuwa unapinga kurejea katika mipaka ya mwaka 1967, bali pia unakataa kurejeshewa Wapalestina eneo la Quds Mashariki na vilevile haki ya wakimbizi wa Palestina ya kurudi katika ardhi zao ambazo hadi sasa  zinakaliwa kwa mabavu na Israel.
Ukweli ni kuwa Kerry ana  matarajio ya kufufua mazungumzo eti ya mapatano kati ya Israel na Wapalestina kwa hali yoyote ile, ambayo yalikwama mwaka 2010 baada ya kuibuka mjadala kuhusu suala la ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi katika ardhi za Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na Quds Mashariki.
Duru mpya ya jitihada za Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani kwa ajili ya kufufua mchakato wa mazungumzo eti ya mapatano kati ya Israel na Wapalestina imeanza katika hali ambayo raia na makundi mengi ya Palestina yanaamini kuwa, mazungumzo hayo yatakuwa na madhara kwa Wapalestina. Vilevile  serikali halali ya Palestina inayoongozwa na Hamas huko katika Ukanda wa Ghaza imetangaza kuwa lengo la safari za mara kwa mara za viongozi wa Marekani akiwemo John Kerry na William Bernz katika eneo la Mashariki ya Kati na katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu na Israel ni kwa ajili tu ya kupoteza muda na kuzipotosha fikra za walio wengi ili kuficha mipango ya ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi katika ardhi za Palestina.
Katika mazingira hayo japokuwa John Kerry Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani analipa kipaumbele suala la kufufua mazungumzo eti ya mapatano kati ya Wapalestina na Israel, lakini inatabiriwa kuwa mazungumzo hayo yatafeli hata kama Mahmoud Abbas Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina pia atakubali kwa mara nyingine tena kushiriki katika mazungumzo hayo na Israel.

No comments: