Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, July 17, 2013

Indhari ya viongozi wa Lebanon kuhusu kuchelewa kuundwa serikali

Nabih Berri, Spika wa Bunge la Lebanon amesema kuwa, mrengo wa Machi 14 umekuwa ukichelewesha uundwaji wa serikali mpya nchini humo. Baada ya kupita miezi minne ya pengo la kisiasa nchini Lebanon udharura wa kuharakisha uundaji wa serikali nchini humo umeongezeka maradufu hasa kwa kutilia maanani anga ya ndani iliyotanda katika nchi hiyo.
Viongozi wa Lebanon wanasema kuwa, kutoundwa serikali mpya nchini humo ni jambo ambalo linaipeleka nchi hiyo upande wa mgogoro na ukosefu wa amani.
Licha ya kupita miezi miwili tangu Tamman Salam alipoteuliwa kuwa Waziri Mkuu wa Lebanon na kutakiwa aunde baraza jipya la mawaziri, lakini ukorofi wa kisiasa na ukwamishaji mambo unaofanywa na mrengo wa Kimagharibi wa Machi 14 unaoongozwa na Saad Hariri umekwamisha hadi sasa kuundwa serikali nchini humo. Ukwamishaji huo wa mambo umekuwa dhahir shahir kiasi kwamba, Nabih Berri Spika wa Bunge la Lebanon amesema kinagaubaga kwamba, mrengo wa Machi 14 wa akina Hariri ndio unaokwamisha kuundwa serikali kutokana na kutoa masharti ya ajabu ajabu na yasiyotekelezeka likiwemo la kutoshirikiswa Hizbullah katika serikali hiyo.
Michel Aoun, Mkuu wa chama cha kikristo cha Free Patriotic Movement amesema kuhusiana na mchakato wa Waziri Mkuu Tammam Salam wa kuunda serikali mpya kwamba, endapo Hizbullah itatupwa nje ya ulingo wa serikali ijayo, basi chama chake pia hakitoshiriki katika serikali hiyo. Tammam Salam aliteuliwa Aprili 6 mwaka huu kwa kura 124 za ndio huku Wabunge wa nne tu wakijizuia kupiga kura. Baada ya uteuzi huo, Waziri Mkuu huyo aliyechukua nafasi ya Najib mikati aliyejiuzulu  alitakiwa kuunda mara moja baraza la mawaziri. Lakini hadi sasa Tammam Salam hajafanikiwa kuunda serikali hiyo. Tammam Salam, mwenye umri wa miaka 67 na ambaye anaungwa mkono na mrengo wa 14 ametoa pendekezo la kuundwa "Serikali ya Maslahi ya Kitaifa" ili makundi yote ya kisiasa yaweze kushirikishwa katika serikali hiyo. Kwa hakika akthari ya shakhsia wa Kilebanoni wanaamini kwamba, mwafaka wa wanasiasa wa Lebanon pekee ndio utakaoweza kukabiliana na njama na uvamizi kutoka nje ya nchi na kuivusha salama nchi hiyo katika kipindi hiki cha mivutano ya kuunda serikali.

No comments: