Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Sunday, June 9, 2013

Kumbukumbu ya miaka 46 ya kukaliwa kwa mabavu Baitul Muqaddas

Sambamba na kutimia miaka 46 ya kukaliwa kwa mabavu Baitul Muqaddas, Wapalestina na wanaharakati wanaounga mkono taifa la Palestina wamefanya maandamano ya kupinga uzayuni katika nchi tofuati duniani na kulaani kukaliwa kwa mabavu Quds Tukufu na kuuyahudishwa mji huo. Jana Ijumaa Juni 7 mwaka 2013 ilisadifiana na kutimia miaka 46 ya kukaliwa kwa mabavu Baitul Muqaddas. Baada ya kughusubu eneo la magharibi mwa Quds mwaka 1948, jeshi la Israel mwaka 1967 pia lilikalia kwa mabavu upande wa mashariki na kuudhibiti kikamilifu mji huo mtukufu.
Kwa mnasaba huo, waandamanaji katika nchi 50 duniani wamelaani hatua hiyo ya Israel na kutaka kukombolewa mji huo na wakaazi wake. Jana wanaanchi wa Misri baada ya swala ya Ijumaa walifanya maandamano makubwa ya kupinga uzayuni katika mji mkuu Cairo, na kuunga mkono taifa la Palestina na kuonyesha mshikamano kwa kadhia ya Quds. Rais Muhammad Mursi wa Misri alisema serikali yake na wananchi sanjari na kulaani jinai za utawala wa Kizayuni, wanaunga mkono kadhia ya Palestina na maslahi ya Wapalestina na kuendelea kufanya jitihada katika uwanja huo. Naye Ahmad Aref msemaji wa kundi la Ikhwanul Muslimin la Misri pia amekosoa jinai na hatua za kibaguzi za Israel dhidi ya Quds, Wapalestina na matukufu yao na kusema kwamba lengo la maandamano hayo ni kuizindua jamii ya kimataifa kuhusiana na suala la Quds, ili paandaliwe mazingira ya kupatikana amani na usalama katika eneo na dunia.  Nchini Mauritania pia wananchi walifanya maandamano ya kupinga uzayuni katika mji mkuu Nouakchott na kuzitaka nchi za Kiarabu na Kiislamu kufanya jitihada hai za kuirejesha Quds kwa wamiliki wake wa asili, kuwafukuza wavamizi na kukomboa mji huo mtukufu. Vilevile maelefu ya wananchi wa Jordan waliandamana jana kwa mnasaba wa kukumbuka kutimia miaka 46 tangu mji wa Baitul Muqaddas ukaliwe kwa mabavu. Kuhusiana na hilo pia Rais Muhammad Wahid wa Maldives jana alipokutana na maafisa wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina huko Ramallah alisema kuwa, msikiti wa al Aqswa ambao ni eneo takatifu siku zote unapaswa kulindwa ili kuzuia kuvunjiwa heshima. Maelfu ya Wapalestina pia sambamba na kufanya maandamano ya kulaani utawala wa Kizayuni katika maeneo tofauti ya Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan walisisitiza kukombolewa mji wa Baitul Muqaddas na msikiti wa al Aqswa kutoka kwa Wazayuni maghasibu. Lakini askari wa Israel waliwashambulia kwa risasi waandamanaji hao katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan ambapo baadhi yao walijeruhiwa. Ismail Haniya Waziri Mkuu wa serikali halali ya Palestina amesema, kadhia ya Palestina ni kadhia ya Kiislamu na kwamba kamwe Wapalestina hawatofumbia macho haki zao zisizopingika kama vile Quds Tukufu na haki ya kurejea wakimbizi wa Kipalestina katika miji na vijiji vyao. Ahmad Abu Jalibah Mkuu wa Kamati ya Quds katika Bunge la Palestina alisisitiza mbele ya waandamanaji wa Ukanda wa Gaza ulazima wa kuimarishwa umoja miongoni mwao ili kukomboa Quds Tukufu kutoka kwa Israel. Maandamano kama hayo pia yamefanyika nchini Uturuki katika miji ya Istanbul na Ankara na pia mjini London Uingereza. Maandamano ya London yalihudhuriwa na baadhi ya wawakilishi wa Bunge la Uingereza, Balozi wa Palestina mjini London na baadhi ya wawakilishi wa taasisi za kisiasa, kiraia na harakati za wanafunzi na wanawake. Utawala wa Kizayuni baada ya kuukalia kikamilifu mji wa Baitul Muqaddas kwa kukiuka maazimio nambari 181, 194 na 242 ya Umoja wa Mataifa, unakusudia kuuyahudisha kabisa mji huo mtukufu, kwa kujenga huko vitongoji vya walowezi wa Kizayuni pamoja na kuwashambulia na kuwafukuza Wapalestina.

No comments: