Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, June 19, 2013

Baraza la Usalama lajadili hali ya watoto vitani

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limefanya kikao kuhusu hali ya watoto katika vita vya silaha, ambapo pia limepokea ripoti ya Katibu Mkuu kuhusu watoto katika vita. Ripoti hiyo imesema, hali ilikuwa mbovu hasa katika kipindi cha miezi 18 iliyopita, wakati mizozo mipya ilipoibuka au ile iliyopo kuenea zaidi.
Akizungumza wakati wa kikao hicho, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu watoto na vita vya silaha, Leila Zerrougui, amesema kuwa, wahusika wasio wa kiserikali katika mizozo wanachangia kwa kiasi kikubwa zaidi ukiukwaji wa haki za watoto.
Miongoni mwa nchi ambazo haki za watoto zimetajwa kukiukwa katika ripoti hiyo ni Mali na Jamhuri ya Afrika ya Kati. Magaidi wanaopata uungaji mkono wa madola ya kigeni nchini Syria, pia wanalaumiwa kutumia watoto vitani.  Nazo Chad na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo zimesifiwa kwa hatua zilizopiga kwa kuonyesha hamu ya kuzingatia maazimio ya Baraza la Usalama na kuweka sheria za kuwalinda watoto katika mizozo. Naye Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kuhudumia Watoto katika Umoja wa Mataifa UNICEF, Yoka Brandt, amesema, lililo muhimu zaidi katika kukomesha ukiukwaji wa haki za watoto katika vita, ni pande zinazozozana kutekeleza majukumu yao vizuri katika kulinda haki za watoto, na wale wanaozikiuka kukabiliwa na mkono wa sheria.

No comments: