Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Tuesday, January 29, 2013

Mkutano wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu wamalizika, Tehran

Mkutano wa 26 wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu ulimaliza shughuli zake jana usiku hapa mjini Tehran. Mkutano huo ulifanyika kwa kaulimbiu ya "Mtume Mtukufu, Nembo ya Utambulisho wa Umma wa Kiislamu" na umewashirikisha wanafikra na wasomi wa Kiislamu kutoka nchi 102.
Taarifa iliyotolewa na wasomi wa Kiislamu wa madhehebu mbalimbali mwishoni mwa mkutano huo imesisitiza juu ya udharura wa kubuniwa njia za kimatendo za kuyakurubisha pamoja madhehebu ya Kiislamu. Washiriki katika mkutano huo wa kimataifa wamesema kuwa kukurubisha pamoja wafuasi wa madhehebu mbalimbali za Kiislamu ndio njia muhimu zaidi ya kufikiwa umoja wa Umma wa Kiislamu na kusisitiza kuwa, Umma wa Kiislamu unapaswa kushikamana na kuwa na umoja kwa shabaha ya kukabiliana na njama za maadui.
Taarifa ya washiriki wa Mkutano wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu imeashiria kuwa Qur'ani Tukufu na Suna za Mtume (saw) vinamtayarishia mwanadamu anga nzuri ya kufikia ustaarabu na ufanisi na kutilia mkazo udharura wa kutumiwa vyema utajiri huo wa Waislamu katika maisha yao.

Mkutano wa 26 wa Umoja wa Kiislamu umeyatambua mapambano ya wananchi wa Palestina dhidi ya utawala ghasibu wa Israel kuwa ni haki yao ya kisheria na umezitaka jumuiya za kimataifa kuufikisha mahakamani utawala huo kwa tuhuma ya kutenda jinai za kivita na jinai dhidi ya binadamu. Taarifa ya washiriki katika mkutano huo pia imelaani ujenzi wa vitongoji vya walowezi wa Kiyahudi katika ardhi za Palestina na kutoa wito wa kuundwa nchi huru ya Palestina mji wake mkuu ukiwa Baitul Muqaddas.
Washiriki pia wamelaani mashambulizi ya kigaidi yanayofanyika katika maeneo mbalimbali ya dunia na kusema kuwa, Uislamu unapinga ugaidi katika sura zake zote.
Wamesisitiza pia juu ya umuhimu wa kubuniwa ufumbuzi wa Kiislamu kwa ajili ya migogoro ya ulimwengu wa Kiislamu hususan mgogoro wa sasa wa Syria.
Kabla ya kusomwa taarifa ya mwisho wa Mkutano wa 26 wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu, Spika wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Dakta Ali Larijani alihutubia mkutano huo akisisitiza juu ya umuhimu wa kuwepo umoja na mshikamano kati ya Waislamu kwa ajili ya kukabiliana na njama za mabeberu. Dakta Larijani amesema kuwa Marekani na nchi za Magharibi zinafanya mikakati ya kuzigawa nchi za Kiislamu na kuongeza kuwa, udhibiti bandia wa Marekani na Magharibi umeporomoka na sasa Waislamu wameanza kupiga hatua za maendeleo. Amesema Umma wa Kiislamu umo katika harakati za kutengeneza historia mpya ya dunia.
Vilevile mshauri wa rais wa Sudan Abdur Rahiim bin Ali amesema katika mkutano huo kwamba, kuna udharura wa kuimarishwa umoja na mshikamano wa Waislamu katika mambo yanayowakutanisha wafuasi wa madhehebu zote kwa shabaha ya kuzima njama za maadui wa Uislamu.
Mkutano wa Kimataifa wa Umoja wa Kiislamu ni miongoni mwa matukio makubwa ya ulimwengu wa Kiislamu na hufanyika kila mwaka hapa nchini ukiwakutanisha wasomi, wanafikra na maulamaa wa madhehebu mbalimbali za Kiislamu kwa lengo la kuimarisha umoja na mshikamano kati ya wafuasi wa madhehebu hizo mbele ya njama na mikakati ya maadui wa umma.

No comments: