Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Tuesday, January 22, 2013

Kifua Kikuu TB

Ahlan Wasahlan wasikilizaji wapenzi na maashiki wa kipindi cha Ijue Afya Yako. Ni matumaini yangu kuwa nyote hamjambo na karibuni katika kipindi kingine ambapo kama tulivyoahidi huko nyuma, kwenye kipindi chetu hiki tutakuwa pia tukizungumzia magonjwa mbalimbali. Katika kipindi chetu cha leo tutazungumzia kuhusu ugonjwa wa kifua kikuu au TB ambao maambukizo yake yanaongezeka kwa kasi kubwa ulimwenguni, khususan katika nchi zinazoendelea. Karibuni  mjumuike nami hadi mwisho wa kipindi.

Kwa kuzingatia kuwa ugonjwa wa Kifua Kikuu huathiri watu wa rika zote na hasa vijana kati ya miaka 15 hadi 45 ambao ndiyo nguvu kazi katika nchi nyingi za dunia, inapasa kufanyika jitihada kubwa za kudhibiti maambukizo ya ugonjwa huo. Kifua Kikuu ambao kitaalamu hujulikana kama Tuberculosis ni ugonjwa wa kuambukiza ambao huenezwa kwa njia ya hewa. Kifua kikuu husababishwa na bacteria au kimelea aina ya Mycobacterium Tuberculosis au (tubercle bacterium). Ugonjwa huu kwa kawaida huathiri mapafu, lakini pia huweza kushambulia viungo vingine vya mwili kama vile tezi za limfu, ubongo na mifupa. Kwanza kabisa hebu tuone ugonjwa wa Kifua Kikuu unambukizwa kupitia njia zipi?

Mtu mwenye Kifua Kikuu au Tb ambaye hajatibiwa anapokohoa, kupiga chafya, kutema mate au makozi husambaza bakteria au vimelea vya ugonjwa huo hewani. Kwa hivyo mtu mwingine akivuta hewa yenye vimelea hivyo anaweza kuambukizwa ugonjwa huo. Kwa mfano takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa nchini Tanzania ugonjwa wa Kifua Kikuu umekuwa ukiongezeka kwa kasi kubwa ambapo watu elfu 65,000 hivi sasa wanaugua kifua kikuu nchini humo. Kati ya hao asilimia 50 pia ni waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi.
Hapa linajitokeza swali kwamba dalili za Kifua Kikuu ni zipi?
Mtu ambaye amepatwa na ugonjwa wa Tb au Kifua Kikuu huwa na dalili au husumbuliwa na hali zifuatazo: Kukohoa kwa muda usiopungua wiki mbili na mara nyingine kukohoa damu, homa za jioni za mara kwa mara, kutokwa na jasho usiku, kukosa hamu ya kula, kupungua uzito kwa kiasi kikubwa na kadhalika.
Kundi ambalo liko kwenye hatari kubwa ya kuambukizwa Tb ni la wale wanaoishi karibu na kwa muda mrefu na mtu ambaye alikwisha ambukizwa ugonjwa huo. Kwa hiyo hapa tutataja makundi ambayo yako kwenye hatari na uwezekano mkubwa wa kuambukizwa Tb iwapo watakuwa karibu na wenye ugonjwa huo. Watu hawa ni rahisi kupatwa na kifua kikuu kwa sababu kinga zao za mwili huwa ni za kiwango cha chini na watu hao ni, watoto wadogo na wazee, watu wanaougua kisukari, watu wanaotumia dawa aina ya steroids au dawa nyinginezo zinazoathiri mfumo wa kinga ya mwili, waathirika wa ukimwi na virusi vya HIV, wale wanaoishi maeneo yenye msongamano mkubwa wa watu yaliyoduni kiafya, wanaoishi kwenye sehemu zisizokuwa na hewa safi ya kutosha, watu wanaotumia dawa mbalimbali, au pombe na pia wale wenye lishe duni.

Wasikilizaji wapenzi na sasa tuangalia ni vipimo gani hutumika kujua iwapo mtu ameambukiza Kifua Kifuu. Vipimo vinavyotumika kwa sasa katika nchi nyingi hususan katika ulimwengu wa dunia ya tatu ili kupima ugonjwa wa Kifua Kikuu ni kipimo cha picha ya kifua au x-ray, kipimo cha makohozi, kipimo cha ngozi au Mantoux test. Iwapo vipimo hivyo vitathibitisha kuwa mtu ameambukizwa Kifua Kikuu, mtu huyo atapaswa kutibiwa kikamilifu kwa kufuata ushauri wa daktari ili kuutokomeza ugonjwa huo. Baada ya kufahamu nini ugonjwa wa Tb, chanzo chake na dalili zake, sasa ni vyema tuelewe ni yapi matibabu yake. Je, Kifua Kikuu kinaweza kutibika? Jibu ni ndiyo. Kuna dawa aina ya antibiotic ambazo ni tiba mujarabu ya kutokomeza Tb lakini zinapaswa kutumiwa kwa kuzingatia ushauri wa daktari. Itakumbukwa kuwa Shirika la Afya Duniani WHO limetoa mwongozo mpya wa kutibu ugonjwa wa Kifua Kikuu kwa kutumia dawa za mseto (fixed dose combination drugs au FDCs) ambazo hutumika sana katika nchi nyingi ulimwenguni ili kupunguza muda wa matibabu kutoka miezi minane hadi sita. Jambo muhimu la kuzingatia katika utumiaji wa dawa hizo ni kuwa, ni vyema mgonjwa atumie dawa hizo kama alivyoshauriwa na daktari au mtaalamu wa afya na kumaliza dozi aliyoandikiwa. Kwa hiyo kuna haja ya mgonjwa kuwa chini ya uangalizi maalumu ili kuruhusu dawa za antibiotic kufanya kazi vyema na kuleta athari nzuri kwa mgonjwa. Pili kuna chanjo ya BCG. Hii ni chanjo ambayo hutolewa kwa mtoto mara baada ya kuzaliwa. Chanjo hii humlinda mtoto na ugonjwa wa Kifua Kikuu. Hata hivyo katika nchi nyingine chanjo hii hutolewa baadaye kwa watoto ambao wako katika hatari ya kuambukizwa ugonjwa huo.  Hebu sasa na tunagalie ni chakula gani anachopaswa kula mgonjwa wa TB. Mgonjwa anayesumbuliwa na Kifua Kifuu anatakiwa kula mlo kamili wenye proteini, vitamini na cabohyadrate. Vyakula vya protini ni pamoja na mayai, maziwa, maharage na soya. Vyakula hivyo hujenga misuli na kuzalisha chembe za damu. Vilevile husaidia mfumo wa kinga ya mwili kupata nguvu. Halikadhalika ni vyema mgonjwa wa TB apate vitamini zitokanazo na mafuta na mboga za majani. Vyakula hivyo huongeza nguvu na kukinga mwili wake hasa ngozi. Chakula aina ya carbohydrate ambayo inapatikana katika vyakula vya nafaka mfano wa mahindi na ngano na vilevile sukari itokanayo na matunda navyo pia vina umuhimu mkubwa. Hii ni kwa sababu vyakula hivyo huleta nguvu katika mwili wa mwanadamu. Vile vile bila kusahau maji safi na salama yanayohitajika mwilini. 

Mnaendelea kutegea sikio kipindi cha Ijue Afya Yako kinachowajia kupitia Idhaa ya Kiswahili Sauti ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Kuna njia mbalimbali za kujikinga na ugonjwa wa Kifua Kikuu au TB ambazo ni kujikinga na ugonjwa huo kunakoanzia kabla ya mtu kupatwa na ugonjwa huo kwa watu wa kaiwada, ambapo chanjo ya kuulinda mwili na ugonjwa huo hutolewa kwa watoto wadogo baada ya kuzaliwa. Chanjo hiyo ya Kifua kikuu huitwa BCG. Njia nyingine ni kuwakinga watu wa familia za wale walio karibu na wanaouguwa ugonjwa wa TB. Kuwakinga wale wenye vijidudu vya ugonjwa wa kifua kikuu mwilini mwao lakini bado dalili za ugonjwa huo hazijajitokeza na kuwakinga wale walio katika hatari ya kupata ugonjwa huo.
Dawa aina ya Isoniazid (INH) inaweza kutumika katika kuzuia Kifua Kikuu kwa wale walio na vijidudu vya ugonjwa huo katika miili yao lakini bado dalili za ugonjwa huo hazijajitokeza. Ugonjwa wa Kifua Kikuu ni ugonjwa unaozuilika kwa kiasi kikubwa. Ili kuwazuia watu wasipatwe na ugonjwa huo inapasa watu walioambukizwa ugonjwa huo wajulikane mapema, hasa wale wanaokabiliwa na hatari kubwa ya kuonyesha dalili ya ugonjwa huo katika siku za usoni. Dawa ya INH inatumika kwa kiasi kikubwa kuzuia watu wasipate ugonjwa wa TB ambao wanaishi karibu na wagonjwa wa Kifua Kikuu au wale wenye uhusiano na wagonjwa hao na wale wenye vimelea vya Tubercle bacilli katika miili yao lakini bado hawajafikia katika hali ya kuwa na TB halisi. Dawa hiyo hupewa na kutumiwa kila siku kwa miezi 12 mfululizo.
Katika nchi zilizoendelea kama vile Marekani, watu wa makundi yafuatayo wanapaswa kupewa dawa za kujikinga, bila kujali umri wao, iwapo huko nyuma hawajawahi kutibiwa ugonjwa wa Kifua Kikuu.
1. Watu ambao wanaishi na kushirikiana na wale walioambukizwa ugonjwa wa kifua kikuu. (zaidi ya hao watoto, na vijana ambao kipimo cha PPD kimeonyesha kuwa hawana ugonjwa huo, lakini kwa miezi mitatu wamekuwa wakiishi au kuwa karibu na wenye ugonjwa huo. Matibabu yanapaswa kuendelea hadi pale kipimo cha ngozi kitakapochukuliwa tena na majibu kuonyesha hawajaambukizwa ugonjwa huo.

2. Watu wengine wanaopaswa kupewa kinga ya BCG ni wale ambao kipimo cha ngozi cha Kifua Kikuu kimeonyesha wana ugonjwa huo, pamoja na wale ambao picha yao ya X-ray inaonyesha wana ugonjwa wa TB ingawa bado hawajaonyesha dalili za ugonjwa huo. (Inactive TB).
3. Watu ambao kipimo cha ngozi cha kifua kikuu kimeonyesha hawana ugonjwa huo lakini pia wanakabiliwa na hatari ya kuambukizwa magonjwa kama vile ya HIV, Kisukari au wale wanaotumia dawa aina ya Corticosteroid.
4. Waathirika wa ugonjwa wa Ukimwi na wale wanaodhaniwa kuwa wameambukizwa virusi vya HIV na ambao wakati wowote huko nyuma kipimo cha ngozi kiliwahi kuonyesha wameambukizwa ugonjwa huo, hata kama hawana dalili.
5. Wale wanaotumia madawa ya kulevya kwa njia ya kujidunga sindano, ambao vipimo vya ngozi vimeonyesha wameambukizwa ugonjwa wa TB, hata kama bado hawana dalili za ugonjwa huo.
Watu wafuatao pia wenye umri wa zaidi ya miaka 35, wanapaswa kupewa dawa za kuzuia Kifua Kikuu: Wale wanaoishi katika maeneo yenye maambukizo mengi ya TB. Watu ambao wanaishi katika mazingira magumu, wale ambao wana kipato cha chini na wanaishi katika maeneo yenye misongamano. Watu ambao wameishi kwa muda mrefu jela, majumba ya kulelea wazee na sehemu za watu wenye matatizo ya kiakili.
Inapaswa kujua kuwa, wafanyakazi wa vitengo vya afya ambao mara kwa mara wanakutana na kuwashughulikia wagonjwa wa Kifua Kikuu wanapaswa kufanyiwa vipimo vya ngozi vya TB kila baada ya miezi 6.
Wagonjwa wenye kifua kikuu wanapaswa kufundishwa kuziba midomo yao na pua pale wanapokohoa au kupiga chafya. Wagonjwa wenye Kifua Kikuu wanapaswa kutengwa na kuwekwa kwenye vyumba ambavyo hewa inabadilika kwa urahisi. Pia wazazi wahakikishe kuwa watoto wao wanapatiwa kinga ya kifua kikuu katika wakati unaotakiwa.
Naam wapenzi wasikilizaji, na kufikia hapo hatuna  la ziada. Ni matumaini yetu kuwa mmefaidika na yale tuliyowaandalia katika kipindi chetu hiki. Hadi wiki ijayo, daima tuzitunze afya zetu na kwaherini.

No comments: