Askari wa jeshi la Polisi mkoani Mtwara nchini Tanzania wamelazimika
kupiga mabomu ya machozi kutwa nzima hapo jana katika kata ya
Chikongola, Manispaa ya Mtwara Mikindani kutawanya wananchi
walioizingira nyumba ya diwani wa kata hiyo Mohamedi Chehako kwa madai
ya kuwahifadhi wachawi ndani ya nyumba yake, huku mwandishi wa habari
mmoja akiripotiwa kujeruhiwa. Habari ambazo hazijathibitishwa na Kamanda
wa Polisi mkoani Mtwara, Maria Nzuki zinadai kuwa majira ya saa 10
kasoro za jioni watu wanaodaiwa kuwa ni wanajeshi wa Jeshi la Wananchi
Tanzania (JWTZ) waliingilia kati na kuanza kutembeza mkong'oto kwa
wananchi ili kuzima vuguvugu hilo.
Aidha wananchi hao waliokuwa na
hasira walichoma moto mahakama ya Mwanzo na kuvunja vioo vya nyumba za
waheshimiwa Hawa AbdulRahman Ghasia Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu
(TAMISEMI) na ya Mohamed Said Sinani Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mtwara.
Wakiwa katika mahakama ya mwanzo, Polisi walizingirwa na vijana
waliokuwa wamebeba mawe na kufunga barabara zote za kuingia na kutoka
Kituo Kikuu cha Mabasi na eneo la Soko Kuu, licha ya kufyatua hewani
mabomu ya machozi. Mkoa wa Mtwara katika wiki za hivi karibuni
umeshuhudia maandamano na mapigano kati ya wananchi na jeshi la Polisi,
kutokana na msimamo wa wananchi kupinga uamuzi wa serikali wa kutaka
kuisafirisha gesi asilia kutoka mkoani humo na kuipeleka Dar es Salaam
kwa njia ya mabomba. Kwa upande mwengine, vurugu kubwa zimezuka katika
eneo la Dumila mkoani Morogoro ambapo wananchi wamechoma moto nyumba na
kupasua vioo vya magari na hivyo kuzuia magari yote yanayotumia
barabara hiyo, kwa madai kuwa wanapinga agizo la Mkuu wa Wilaya hiyo la
kuwanyang'anya ardhi Wakulima na badala yake wamepewa Wafugaji. Vurugu
hizo zimesababisha kifo cha mtu mmoja na wengine kadhaa kujeruhiwa.Saturday, January 26, 2013
Machafuko Mtwara, Morogoro, Mahakama yachomwa moto
Posted by
AO Secretarial & Technology Supplies
Labels:
Machafuko Mtwara,
Mahakama yachomwa moto,
Morogoro
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment