Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Sunday, February 8, 2015

Kutangazwa katiba mpya ya mpito kwa ajili ya kutatua mgogoro wa kisiasa wa Yemen

Kufuatia kuvunjika mazungumzo ya kitaifa kati ya makundi ya kisiasa kwa lengo la kufikiwa makubalino ya kitaifa nchini Yemen, hapo jana Ijumaa tume ya mapinduzi sanjari na kuitisha kongamano lililoyahusisha makundi tofauti ya kisiasa, kiuchumi, kijamii na kielimu, ilitangaza katiba mpya ya mpito ambayo inatazamiwa kumaliza hali ya mchafukoge nchini humo. Kwa mujibu wa taarifa ya ikulu ya rais mjini Sana’a iliyotangazwa kupitia televisheni ya taifa, katiba hiyo ya mpito, inajumuisha kuundwa baraza la rais wa nchi na baraza la kitaifa kwa minajili ya kumaliza mgogoro wa taifa hilo.
Mawazi wa Mambo ya Ndani na Ulinzi na hali kadhalika viongozi wa idara ya usalama, ni miongoni mwa waliohudhuria kikao hicho katika ikulu ya rais. Katiba hiyo ya mpito na baraza la rais nchini Yemen, vitaliongoza taifa hilo kwa kipindi cha miezi mitatu toka sasa. Kabla ya hapo na katika mazungumzo yaliyofanyika mjini Sana’a makundi ya kisiasa, yalikubaliana, kuunda baraza la rais lenye shakhsia watano ambalo litakuwa chini ya Ali Nasir Muhammad rais wa zaman wa Yemen ya Kusini kabla ya nchi hiyo kuungana na ya Kaskazini hapo mwaka 1990. Kabla ya hapo yaani siku ya Alkhamis iliyopita tume hiyo ya mapinduzi ilikuwa imetangaza kuwa, kufuatia kuvunjika mazungumzo ya kisiasa ingetangaza katiba ya mpito chini ya usimamizi wa Jamal Benomar, mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa nchini humo. Kwingineko duru za habari zimeripoti kuwasili Benomar, nchini Saudia kabla ya kutangazwa katiba hiyo. Huku hayo yakijiri, tume ya mapinduzi nchini humo, imetangza kuvunjwa kwa baraza la wawakilishi na badala yake kuundwa baraza la mpito linalowajumuisha wabunge 551. Mmoja wa wawakilishi wa tume ya wananchi amenukuliwa akisema kuwa, kutangazwa katiba mpya nchini Yemen, kumeonyesha matunda ya kikao cha mapinduzi na kuongeza kwamba, katiba hiyo ni kwa madhumuni ya kufikiwa uhuru na utukufu wa Wayemen wote. Ameongeza kuwa, mapinduzi ya wananchi hayakuwa bila faida na kwamba, wananchi wote wa taifa hilo wanapasa kujitolea kwa ajili ya kuisafisha nchi yao kutokana na mafisadi sanjari na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria, hasa kwa kutilia maanani kwamba lengo la mapinduzi hayo lilikuwa ni kuleta marekebisho nchini humo. Muhammad al-Bakhiti, mwakilishi wa Baraza la Kisiasa la Harakati ya Answarullah nchini Yemen, ameitaja pia katiba hiyo kuwa njia ya kutatuliwa mgogoro wa kisiasa nchini humo na kusisitiza kuwa, chama cha mrengo wa marekebisho chenye mafungamano na kundi la Ikhwanul Muslimin na baadhi ya makundi mengine, ndio chanzo cha kufeli mazungumzo ya kisiasa nchini, hasa kutokana na mirengi hiyo kufuata amri kutoka nje. Inatazamiwa kuwa, kutangazwa katiba ya mpito nchini Yemen, kutaweza kuhitimisha mgogoro wa kisiasa nchini humo sanjari na kufanikisha kuundwa serikali ya wananchi itakayozijumuisha shakhsia mbalimbali na kuundwa Yemen moja yenye nguvu na iliyo na shikamano imara wa kitaifa. 

No comments: