Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, June 2, 2014

Al-Sisi kuapishwa J'mosi ijayo kuwa rais mpya Misri

Abdul Fattah al Sisi, kiongozi wa kijeshi aliyeongoza mapinduzi ya kijeshi dhidi ya rais aliyechaguliwa na wananchi Muhammad Mursi, ataapishwa siku ya Jumamosi ijayo kama rais mpya wa Misri. Duru za habari zimewanukuu maafisa wa vyombo vya mahakama nchini Misri wakisema leo kwamba, tume ya uchaguzi wa rais uliofanyika hivi karibuni nchini humo, itatangaza matokeo rasmi ya uchaguzi huo siku ya Jumanne.
Hii ni katika hali ambayo kwa mujibu wa matokeo yasiyo rasmi ya uchaguzi huo, kiongozi huyo wa kijeshi na waziri wa zamani wa ulinzi wa nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika, ameshinda kwa zaidi ya asilimia 93 ya kura.
Uchaguzi wa rais nchini Misri ulifanyika wiki iliyopita kwa ushiriki dhaifu wa wananchi baada ya kususiwa na vijana walio wengi ambao ndio walioongoza harakati za mapinduzi dhidi ya utawala wa dikteta Hosni Mubarak mwaka 2011.
Wakati huo huo mahakama moja nchini Misri leo imesikiliza kesi ya Mubarak na wanawe wawili Alaa na Gamal katika kesi maarufu inayoitwa 'kesi ya karne' ambapo watuhumiwa hao walifikishwa kizimbani. Katika kesi hiyo Mubarak na wanawe wanatuhumiwa kufanya mauaji dhidi ya waandamanaji katika maandamano ya amani na pia kutokana na kuiingizia hasara ya mabilioni ya fedha Misri kutokana na kuuzia utawala haramu wa Kizayuni gesi ya nchi hiyo kwa bei ya kutupa.

No comments: