Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Thursday, May 22, 2014

Waislamu Nigeria wachukizwa na jinai za Boko Haram

Waislamu nchini Nigeria wameeleza kuchukizwa kwao na vitendo vinavyoendelea kufanywa na kundi la Boko Haram la nchi hiyo na kulaani vikali kuhusishwa vitendo hivyo vichafu na dini tukufu ya Kiislamu. Waislamu nchini Nigeria jana walikusanyika katika Msikiti Mkuu wa Abuja na kumuomba Mwenyezi Mungu ili wasichana zaidi ya 250 wanaoshikiliwa mateka na kundi la Boko Haram waachiliwe huru. Sheikh Mussa Muhammad Imam wa msikiti huo amesema kuwa, dini ya Kiislamu inapinga vikali kitendo cha kuwaua watu wasio na hatia.
Sheikh Mussa Muhammad ameongeza kuwa, dini tukufu ya Kiislamu pia haimlazimishi mtu kufuata dini hii bila ya ridhaa yake. Imam wa Msikiti Mkuu wa Abuja amesema kuwa, kundi la Boko Haram haliwalengi na kuwaua Wakristo pekee, bali hata Waislamu wamekuwa wakiuawa na kushambuliwa na kundi hilo. Waislamu waliokusanyika jana kwenye Msikiti Mkuu wa Abuja wamesema kuwa, kundi la Boko Haram linatafsiri visivyo Qurani  Tukufu na Jihadi, na  kwamba vitendo vinavyofanywa na kundi hilo ikiwa ni pamoja na kuwaua watu wasio na hatia, uripuaji na uchomaji moto nyumba  za wanavijiji, ni kinyume na mafundisho ya dini ya Kiislamu. Inafaa kuashiria hapa kuwa, miaka kadhaa iliyopita, maulamaa kadhaa wa Kiislamu waliuawa kinyama baada ya kulikosoa kundi hilo.

No comments: