Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Friday, May 23, 2014

Marekani kutuma wataalamu wa kijeshi nchini Chad

Rais wa Marekani ameliandikia barua Baraza la Kongresi la nchi hiyo juu ya mpango wa kutumwa wataalamu 80 wa kijeshi wa nchi hiyo huko Chad. Kwa mujibu wa madai ya Rais Barack Obama, wanajeshi hao wa Marekani watapelekwa nchini Chad kwa shabaha ya kuisaidia serikali ya Nigeria kwenye operesheni ya kuwaokoa wanafunzi wasichana 276 wanaoshikiliwa mateka na wanamgambo wa kundi la Boko Haram la nchi hiyo. Kundi la Boko Haram liliwateka nyara wanafunzi hao wa shule ya bweni kwenye mji wa Chibok ulioko kwenye jimbo la Borno kaskazini mashariki mwa nchi hiyo mwezi uliopita. Wanamgambo hao walitishia kwenye mkanda wa video waliourusha hewani kwamba, watawauza kama vijakazi wasichana hao kwenye nchi za Cameroon na Chad. Serikali ya Nigeria kuanzia mwezi Mei mwaka jana ilitangaza hali ya hatari kwenye majimbo manne yaliyoko kaskazini mashariki mwa nchi hiyo, kwa shabaha ya kupambana na kundi hilo. Hadi sasa operesheni za kigaidi katika maeneo hayo zingali zinaendelea na kusambaa hadi Abuja, mji mkuu wa Nigeria. Mara baada ya kutekwa nyara wanafunzi hao, serikali ya Nigeria haikuchukua hatua zozote muhimu za kuwakomboa wanafunzi hao, hadi pale wananchi walipoandamana na kupasa sauti zao zilizosikika pembe mbalimbali ulimwenguni kupitia mitandao ya kijamii. Hii ni katika hali ambayo, licha ya kutekwa nyara wanafunzi hao, miripuko ya mabomu iliyotokea hivi karibuni katika mji wa Jos na kupelekea watu wasiopungua 150 kuuawa, imeandaa mazingira kwa madola ya Magharibi kuingilia masuala ya ndani ya nchi hiyo. Rais Francois Hollande wa Ufaransa wiki iliyopita kwa kutumia kisingizio cha masuala ya kibinadamu, aliitisha kikao mjini Paris, kilichowashirikisha wakuu wa nchi za Nigeria, Niger, Cameroon, Chad na Benin kwa lengo la kujadili usalama wa Magharibi mwa Afrika na hasa kuhusiana na  kadhia ya kutekwa nyara wanafunzi wasichana nchini Nigeria. Kwenye mazungumzo hayo, Rais Hollande alitahadharisha juu ya kutokea vita barani Afrika vitakavyosababishwa na jinai za kigaidi za Boko Haram. Rais wa Ufaransa amewaomba wakuu wa nchi tano za Kiafrika zinazopakana na Nigeria, watekeleze operesheni za pamoja kwa lengo la kuliangamiza kundi hilo. Vyovyote itakavyokuwa, serikali ya Nigeria haiwezi kulitokomeza kundi la Boko Haram, bila ya kushirikiana kijeshi na kiusalama na nchi majirani. Lakini hivi sasa, serikali ya Nigeria iko ukingoni mwa gema kubwa na kama viongozi wake watakosea kwenye mahesabu yao, wataibadilisha nchi hiyo na kuwa kambi ya majeshi ya nchi za Magharibi. Ufaransa, Uingereza na Marekani kwa kuitumia fursa hii iliyopo hivi sasa, zinafanya juhudi za kulishikia bango suala la mashambulio ya kigaidi ya Boko Haram ili ziweze kupeleka majeshi yao nchini humo. Makundi kama Boko Haram yamekuwa yakiundwa na Wamagharibi, kwa lengo la kuzusha ghasia na machafuko na hatimaye kuichafua taswira ya dini tukufu ya Kiislamu. Hii ni katika hali ambayo, mashambulio yanayofanywa na kundi la Boko Haram kwenye misikiti, makanisa na dhidi ya raia wasio na hatia, yako mbali kabisa na fikra na mafundisho ya dini tukufu ya Kiislamu. Mauaji dhidi ya watu wasio na hatia kaskazini mwa Nigeria, kidhahiri yanaonekana kufanyika kwa jina la Uislamu, lakini kiundani ni operesheni na mkakati maalumu uliopangwa kwenye miaka ya hivi karibuni kwa lengo la kuuogopesha Uislamu, ili Marekani na washirika wake yaani Uingereza na Ufaransa waweze kufanikisha malengo yao haramu barani Afrika.

No comments: