Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Tuesday, May 20, 2014

"Maafa ya kibinadamu yanaijongelea Somalia"

Kiongozi mwandamizi wa Umoja wa Mataifa amesema kuwa, kuna uwezekano mkubwa kwa Somalia kutumbukia kwenye mgogoro mkubwa wa hali mbaya ya kibinadamu kutokana na kupungua misaada ya kibinadamu nchini humo. Philiphe Lazzarini, Mratibu wa masuala ya misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia amesema kuwa, upungufu mkubwa wa chakula, kushadidi maradhi mbalimbali na ukosefu mkubwa wa usalama ni miongoni mwa mambo yatakayoitumbukiza nchi hiyo kwenye majanga makubwa ya kibinadamu. Lazzarini ameongeza kuwa, karibu watu milioni mbili na nusu wanakabiliwa na uhaba wa chakula, lishe duni na maradhi nchini Somalia.
Afisa huyo mwandamizi wa Umoja wa Mataifa amesisitiza kuwa, iwapo hazitachukuliwa hatua za haraka, Somalia itakabiliwa na majanga kama yale yaliyoikumba nchi hiyo mwaka 2011. Ofisi ya Mratibu wa masuala ya misaada ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa ilizitaka nchi wanachama wa umoja huo kukusanya jumla ya dola milioni 933 kwa minajili ya kutekelezwa operesheni ya dharura ya kutuma misaada ya kibinadamu nchini Somalia. Lazzarini amebainisha kuwa, hadi sasa ni kiasi cha dola milioni 170 tu ndicho kilichokusanywa kutoka kwa nchi wanachama.

No comments: