Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, May 21, 2014

Heka heka za Jeshi katika kukaribia kushika tena madaraka nchini Misri

Matokeo ya awali ya kura za urais zilizopigwa na Wamisri waishio nje ya nchi yanaonyesha wazi kwamba, jeshi la nchi hiyo karibuni hivi litachukua tena madaraka katika nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika. Duru zinaripoti kwamba, mkuu wa zamani wa jeshi Abdul-Fattah al-Sisi amepata takriban asilimia 90 ya kura zilizohesabiwa za Wamisri waishio nje ya nchi. Ingawa matokeo hayo hayajatangazwa rasmi lakini wapembuzi wa mambo wanasema mipango ya nyuma ya pazia inaendelea kupangwa kati ya al-Sisi na viongozi wa sasa katika serikali ya mpito ya nchi hiyo.
Weledi wa mambo wanaamini kwamba al-Sisi mwisho wa siku ataibuka na ushindi na anachosubiri kwa sasa ni uchaguzi mkuu wa rais kwa Wamisri walioko nyumbani. Zoezi hilo linatarajiwa kufanyika Mei 26 na 27 yaani baadaye wiki ijayo.
Wafuatiliaji wa siasa za Misri wanasema uchaguzi huo ni wa kimaonyesho tu kwani mahesabu yake yalipangwa na kuratibiwa kitambo na kwamba matokeo yake tayari yashajulikana hata kabla ya upigaji kura ndani ya Misri kuanza. Wachanganuzi hao wanasema kuweko wagombea wawili tu wa urais kwenye uchaguzi wa Misri ambapo mmoja wao ni mwanajeshi wa zamani ni ishara tosha kwamba jeshi linajiandaa kurudi tena madarakani baada ya kamanda wao mkuu, Hosni Mubarak kuangushwa na wananchi mwaka 2011.
Jenerali Abdul-Fattah al-Sisi ambaye anapigiwa upatu kushinda kwenye uchaguzi huo amekuwa akisema lengo lake la kugombea urais ni kutaka kukabiliana na umasikizi, kurejesha usalama ndani ya Misri pamoja na kuimarisha uchumi unaoyumba wa nchi hiyo. Mapendekezo kama hayo pia yametolewa na mgombea wa pili wa urais wa Misri, Hamdeen Sabahi ambaye wadadisi wengi wa kisiasa wanasema amewekwa na jeshi kwenye kinyang'anyiro hicho ili kuonyesha kuna ushindani na demokrasia nchini.
Hapana shaka kuwa, jeshi limekuwa na satua kubwa katika siasa za Misri kwa muda mrefu na baada ya kuangushwa utawala wa dikteta Hosni Mubarak mwaka 2011, jeshi hilo lililazimika kujifungia faraghani na kuandaa mikakati mipya ya kurudi tena katika safu za juu za uongozi wa taifa hilo. Weledi wa mambo wanasema rais aliyepinduliwa Dkt. Mohammad Morsi alishindwa kuimarisha uchumi kutokana na hujuma za wazi za maafisa wa jeshi. Hujuma hizo zilikuwa sehemu ya mpango wa kufelisha utawala wa Dkt Morsi ili wananchi waliokuwa na matumaini makubwa kwake waanze kumpinga na kisha kumuondoa madarakani. Kwa kiwango fulani, jeshi lilifanikiwa kufikia lengo hilo.
Yote hayo yakiwa tisa, kumi ni kwamba, kurudi tena jeshi la Misri katika medani ya siasa za nchi hiyo kumetokana na ridhaa ya Wamagharibi wakiongozwa na Marekani. Daima nchi za Magharibi zimekuwa zikitaka jeshi liendelee kutawala huko Misri ili kulinda maslahi ya utawala haramu wa Israe na ndio maana hata baada ya jeshi kumpindua rais aliyechaguliwa kihalali na wananchi, Mohammad Morsi, nchi hizo hazikulaani moja kwa moja mapinduzi hayo. Ili kujitoa kimasomaso zilitoa vitisho visivyotekelezeka dhidi ya majenerali lakini nyuma ya pazia ziliendelea kuunga mkono harakati za jeshi za kurejea tena madarakani katika sura inayoonekana kuwa ya kidemokrasia. 

No comments: