Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Friday, May 16, 2014

Harakati ya Umoja wa AZAWAD yasema iko tayari kuzungumza na serikali ya Mali

Harakati ya Baraza Kuu kwa Ajili ya Umoja wa Azawad (HCUA) imetangaza kuwa iko tayari kufanya mazungumzo na viongozi wa serikali ya Mali. Harakati hiyo aidha imesema iko tayari kuitambua rasmi bendera ya taifa na kuheshimu makubaliano ya amani yaliyotiwa saini tarehe 18 Juni mwaka jana nchini Burkina Faso. Wataalamu wa mambo wana matumaini kwamba misimamo hiyo iliyoonyeshwa na harakati ya Baraza Kuu kwa Ajili ya Umoja wa Azawad itaandaa mazingira ya kurejea kwa kiwango fulani amani na uthabiti nchini Mali.
  Kabla ya hapo kusainiwa makubaliano ya amani na kufanyika uchaguzi wa rais na bunge havikuweza kusaidia kuleta utulivu na uthabiti wa kudumu huko kaskazini mwa nchi hiyo. Harakati ya HCUA ni moja ya makundi ya Watuareg yanayobeba silaha. Harakati hiyo imeitaka Jamii ya Kimataifa ipendekeze mpatanishi na kuitisha mazungumzo katika nchi isiyopendelea upande wowote. Harakati ya Umoja wa Azawad aidha imetangaza kwamba baada ya kufanyika mazungumzo itahakikisha harakati na makundi mengine yote yanayojulikana kuwa ni wapinzani wa serikali ya Mali yanaunganishwa na harakati hiyo. Itakumbukwa kuwa huko nyuma wawakilishi wa makundi yanayobeba silaha ya Watuareg likiwemo hilo la Baraza Kuu kwa Ajili ya Umoja wa Azawad, harakati ya Taifa ya Ukombozi wa Azawad (MNLA), harakati ya Waarabu wa Azawad (MAA) pamoja na makundi mengine mawili ya vikosi vya watani na vya muqawama yalisaini hati ya maelewano na kuahidi kukomesha utumiaji nguvu na mabavu kama njia ya kubainisha maoni na mitazamo yao. Wawakilishi wa makundi yote hayo walisisitiza pia juu ya hamu yao ya kuona amani inarejea nchini Mali.
Viongozi wa serikali ya Bamako wamekaribisha wazo la kufanyika mazungumzo na kueleza kwamba mtazamo wa utumiaji mabavu unakwamisha maendeleo ya eneo zima. Waziri Mkuu wa Mali Moussa Mara ametilia mkazo juu ya kufikiwa maridhiano ya kitaifa kati ya serikali na makundi ya upinzani yanayobeba silaha na kupatikana mwafaka wa kisiasa ili kuhitimisha mgogoro wa kaskazini mwa nchi hiyo. Wakati huohuo kuna ripoti kwamba mazungumzo yamefanyika kati ya makundi yanayobeba silaha nchini Mali na maafisa wa serikali ya Algeria ili kuandaa utangulizi wa mazungumzo ya maridhiano ya kitaifa nchini Mali. Katika upande mwengine baadhi ya wakosoaji wanamtuhumu Rais Aboubakr Keita wa Mali kwa kupoteza fursa ya kuutatua kwa njia ya amani mgogoro wa nchi hiyo. Kwa mtazamo wa wakosoaji hao, Keita hakuheshimu makubaliano ya usitishaji vita na makundi ya upinzani. Wachambuzi wa mambo wana matumaini kuwa mabadiliko ya baraza la mawaziri yaliyofanyika tarehe 5 Aprili na kuteuliwa Moussa Mara kuwa Waziri Mkuu mpya vitafungua njia ya kuhimitisha harakati za wanamgambo wa Kituareg huko kaskazini mwa Mali. Kabla ya mapinduzi ya kijeshi ya mwezi Machi 2012 Mali ilikuwa moja ya nchi zenye demokrasia yenye uthabiti mkubwa zaidi katika eneo la magharibi mwa Afrika. Lakini kukosekana kwa serikali yenye nguvu kulifungua njia kwa makundi ya upinzani yanayobeba silaha kushika hatamu za utawala wa nchi hiyo

No comments: