Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, December 18, 2013

Jaribio la mapinduzi ya kijeshi yaliyofeli Sudan Kusini

Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini ametangaza habari ya kugunduliwa njama ya jaribio la mapinduzi ya kijeshi yaliyofeli nchini humo. Kiir ametangaza kuwa vikosi vya usalama vya Sudan Kusini vimefanikiwa kugundua na kuzima njama za jaribio hilo la mapinduzi ya kijeshi dhidi ya serikali yake. Katika hali ambayo hakuna taarifa za uhakika na kamili zilizopatikana hadi sasa kuhusu njama za jaribio hilo la mapinduzi, weledi wa mambo wanaamini kuwa kitendo hicho kimetekelezwa katika muendeleo wa mashindano ya kuwania madaraka huko Sudan Kusini.
Rais Salva Kiir Mayardit amesisitiza kuwa Rick Machar Makamu wake wa zamani ni miongoni mwa watu waliotiwa mbaroni kwa tuhuma za kupanga jaribio hilo la mapinduzi ya kijeshi. Rick Machar ambaye alifukuzwa kazi tarehe 25 mwezi Julai kwa amri ya Rais wa Sudan Kusini, alikuwa tayari ametangaza nia yake ya kuwa mgombea katika uchaguzi wa rais uliopangwa kufanyika nchini humo mwakani, kabla ya hata ya kuuzuliwa. Weledi wa masuala ya kisiasa wanasema kuwa Rick Machar ameuzuliwa uongozi ili kufuta upinzani wa shakhsiya huyo kwa Salva Kiir Mayardit katika uchaguzi ujao. Baadhi ya duru za habari zilionyesha kutiwa shaka na hatua ya kufutwa kazi Makamu wa Rais Rick Machar na mawaziri wengine wawili wa serikali ya Sudan Kusini na kuhoji kama ilikuwa ni ya kulifanyia marekebisho baraza la mawaziri au kuanza mgogoro wa kisiasa nchini humo. Kwa mtazamo huo, vita vya kuwania madaraka kati ya mwanasiasa Rick Machar na Rais Salva Kiir Mayardit, vinaonekana kuwa na historia ya tangu huko nyuma. Vita vya kuwania madaraka kati ya mahasimu hao wawili wa zamani huwenda vikaisababishia mgogoro wa muda mrefu Sudan Kusini nchi iliyoasisiwa hivi karibuni.
Sudan Kusini ilitangazwa kuasisiwa na kuwa nchi huru tarehe 9 mwezi Julai mwaka 2011.  Weledi wa mambo wanaamini kuwa kujitenga Sudan Kusini na Sudan ni matokeo ya ushawishi wa Marekani na utawala wa Kizayuni pande ambazo zilifanya kila zilichoweza kuigawa vipande  Sudan lengo likiwa ni kudhamini maslahi haramu ya Washington na utawala unaopenda kujitanua wa Tel Aviv. Hasa ikizingatiwa kwamba utajiri mkubwa wa maliasili ya mafuta ya Sudan upo Sudan Kusini na nchi hiyo inahitaji taasisi za mafuta zilizoko Sudan kwa ajili tu ya kuchimba na kupitishia mafuta ghafi yake. Utawala ghasibu wa Israel daima umekuwa ukitoa zingatio maalumu kwa bara la Afrika na maeneo yake ya kiistratejia. Nchi kama Uganda, Kenya na Ethiopia ni miongoni mwa waitifaki wa Israel katika eneo la Mashariki mwa Afrika zenye nafasi muhimu katika siasa za nje za utawala wa Kizayuni.  Katika mgawanyo wa kijiografia wa bara la Afrika, eneo linalozijumuisha Sudan, Kenya, Uganda na Tanzania pamoja na nchi nne za eneo la Pembe ya Afrika, zinajulikana kwa jina la"Afrika Mashariki Kubwa." Eneo hilo pia limekuwa na nafasi makhsusi katika siasa za nje za Marekani. Hii ni kwa sababu Afrika Mashariki Kubwa kwa kuwa na Ghuba ya Aden, bahari Nyekundu na ya Hindi linatambuliwa kuwa mhimili mkuu wa njia za kimataifa za biashara ya mafuta. Kwa hiyo si jambo lililo mbali kwamba mkono wa Marekani na utawala wa Kizayuni ukawa uko nyuma ya pazia la matukio ya ndani yanayojiri hivi sasa huko Sudan Kusini.

No comments: