Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Sunday, July 14, 2013

Marekani inataka mazungumzo ya ana kwa ana na Iran

Serikali ya Marekani inapanga kuwasiliana na rais-mteule wa Iran na kumjulisha azma ya Washington ya kufanya mazungumzo ya ana kwa ana kuhusu miradi ya kuzalisha nishati ya nyuklia ya Jamhuri ya Kiislamu.
Press TV imenukulu ripoti ya gazeti la Marekani la The Wall Street Journal ambalo limeandika kuwa, maafisa wa Marekani Jumanne ijayo wanakutana na wawakilishi wa nchi zingine nne wanachama wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ili kujadili njia za kuamiliana na rais-mteule wa Iran kuhusu kadhia ya nyuklia.

Iran imekuwa ikifanya mazungumzo na kundi la 5+1 ambalo linazikutanisha pamoja Marekani, Uingereza, Ufaransa, Uchina na Russia pamoja na Ujerumani. Mazungumzo hayo yamehusu masuala kadhaa huku kadhia muhimu zaidi ikiwa ni miradi ya nyuklia ya Iran yenye malengo ya amani. Mkuu wa Sera za Kigeni katika Umoja wa Ulaya Catherine Ashton Ijumaa  ya jana alisema kundi la 5+1 linataka hatua imara zichukuliwe katika mazungumzo na Iran.
Marekani, Israel na baadhi ya waitifaki wao wamekuwa wakiituhumu Iran kuwa ina malengo ya kijeshi katika miradi yake ya kuzalisha nishati ya nyuklia. Iran imekanusha madai hayo na kusema shughuli zake za nyuklia zinafanyika kwa malengo ya amani katika fremu ya sheria za kimataifa na chini ya usimamizi wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki IAEA.

No comments: