Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, July 15, 2013

Maandamano dhidi ya serikali nchini Ethiopia

Hii leo makundi ya upinzani nchini Ethiopia yameitisha maandamano makubwa dhidi ya serikali ya nchi hiyo. Kufanyiwa marekebisho sheria na uhuru wa raia, kuheshimiwa katiba na kutekelezwa usawa wa kijamii, ni miongoni mwa matakwa ya wapinzani hao. Inasemekana kuwa, sambamba na polisi kutoa onyo dhidi ya wapinzani, imechukua pia hatua kali za kiusalama kwa ajili ya kukabiliana na maandamano hayo. 
Uingiliaji wa muda mrefu ndani ya masuala ya kidini unaofanywa na serikali ya Addis Ababa, umeibua hasira za wafuasi wengi wa dini mbalimbali nchini humo. Itakumbukwa kuwa, Ijumaa iliyopita maelfu ya Waislamu nchini humo waliandamana kulalamikia hatua ya serikali ya kuingilia mambo yao. Maandamano hayo yalienda sambamba na kumbukumbu ya kutiwa mbaroni na maafisa usalama wa Ethiopia, makumi ya Waislamu na viongozi wao nchini humo. Itakumbukwa kuwa, tarehe 12 Julai mwaka jana maafisa usalama wa nchi hiyo, walivamia msikiti wa An-war ambao ndio msikiti mkubwa zaidi mjini Addis Ababa na kuwatia mbaroni idadi kubwa ya Waislamu wakiwemo masheikh. Hii ni katika hali ambayo, hadi sasa Waislamu hao bado wanaendelea kuteseka katika korokoro za vyombo vya usalama vya Ethiopia. Serikali ya Ethiopia inadai kwamba, Waislamu 74 waliotiwa mbaroni Julai 12 mwaka jana walitenda kosa la uchocheaji wa vurugu. Waislamu nchini humo wanaunda karibu asilimia 34 ya jamii ya raia milioni 85 ya nchi hiyo. Kimsingi ni kuwa, katiba ya nchi hiyo ni ya kisekula isiyoheshimu dini, hata hivyo viongozi wa serikali ya Addis Ababa wamekuwa wakichukua hatua za ubaguzi dhidi ya Waislamu na kuwapendelea wafuasi wa dini nyinginezo, suala ambalo linawakasirisha sana Waislamu. Watu wengi walikuwa na matarajio ya kupatikana mabadiliko chanya katika uwanja wa kisiasa nchini humo baada ya kufariki dunia Meles Zenawi, Waziri Mkuu wa zamani wa nchi hiyo, na mahala pake pamechukuliwa na Hailemariam Desalegn. Hii ni katika hali ambayo, kamata kamata ya hivi karibuni inayotekelezwa na serikali ya Desalegn, Waziri Mkuu wa hivi sasa wa Ethiopia, inatajwa kuwa ni mwendelezo wa siasa za waziri mkuu aliyemtangulia Meles Zenawi. Taasisi mbalimbali za kutetea haki za binaadamu, zinaituhumu serikali ya Zenawi kwa kuwapendelea wananchi wachache wakiwamo Wasomalia wa huko mashariki mwa eneo la Ogaden na kuwafanyia ukandamizaji mkali wapinzani. Ni vyema kuashiria hapa kwamba, Meles Zenawi alikuwa ni mwitifaki mkubwa wa Marekani na alikuwa na ushawishi mkubwa katika mabadiliko ya kwenye nchi kama Sudan, Somalia na kadhalika. Baada ya kuingia madarakani waziri mkuu mpya huko Somalia, mashirika ya kutetea haki za binaadamu kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa la Msamaha Duniani Amnesty International, yaliitaka serikali ya Addis Ababa kutumia fursa iliyojitokeza, kufanya mabadiliko muhimu na kulinda haki za binaadamu nchini humo. Aidha mashirika hayo yametaka kusitishwa utekelezaji wa sheria ya kupambana na ugaidi iliyopitishwa na Zenawi mwaka 2009 nchini Ethiopia.

No comments: