Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Sunday, June 9, 2013

Sisitizo la Kiongozi Muadhamu kuhusu Umoja wa Waislamu

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema koo na ulimi wa wale wanaotoa wito wa umoja miongoni mwa Waislamu ni koo ya Mwenyezi Mungu na koo na ulimi unaoibua  uhasama miongoni mwa Waislamu na madhehebu za Kiislamu ni ulimi wa shetani.
Ayatullahil Udhma Sayyid Ali Khamenei aliyasema hayo Jumamosi wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na maustadh, maqarii na mahafidh wa Qur'ani Tukufu walioshiriki kwenye Mashindano ya 30 ya Kimataifa ya Qur'ani Tukufu yaliyofanyika hapa mjini Tehran. Katika hotuba yake, Kiongozi Muadhamu amesema moja kati ya maamrisho muhimu ya Qur'ani Tukufu kwa Waislamu ni kuwataka wadumishe umoja na mashikamano.
Ameongeza kuwa kujifundisha maarifa ya Qur'ani ni jambo ambalo huandaa mazingira ya kufikia usalama, amani, heshima na kuimarika zaidi maisha ya Waislamu katika kivuli cha mafundisho ya Qur'ani Tukufu. Kiongozi Muadhamu pia amesisitiza ulazima wa Waislamu kujikurubisha na kuifahamu zaidi Qur'ani Tukufu pamoja na maarifa yake yenye kuleta saada. Ameongeza kuwa kati ya maamurisho ya Qur'ani ni kuwataka Waislamu washikamane kwa kamba ya Mwenyezi Mungu na wasifarakiane. Amesema mkabala ya hilo ni njama na mbinu za mabeberu za kuibua hitilafu katika Umma wa Kiislamu na kushadidisha taasubi za kimadhehebu. Kiongozi Muadhamu ameashiria namna baadhi ya tawala na serikali za nchi za Kiislamu zilivyohadaiwa na kuingia katika mtego wa adui na kusema umoja na mshikamano wa Waislamu ni faradhi ya dharura. Kiongozi Muadhamu amesema utawala wa Kizayuni ndio unaofaidika na umwagikaji damu na hitilafu katika umma wa Kiislamu. Ayatullah Khamenei pia ameashiria wimbi la chuki dhidi ya Uislamu linaloongozwa na nchi za Magharibi na kusema adui wa Kimagharibi amewaelekezea Waislamu upanga na hivyo Umma wa Kiislamu unapaswa kujiimarisha ili kukabiliana na hali hiyo.

No comments: