Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Tuesday, January 29, 2013

Maandamano ya kwanza ya wapinzani nchini Zambia

Kwa mara ya kwanza serikali ya Zambia imewapa wafuasi wa chama cha upinzani kibali cha kufanya maandamano katika mji mkuu wa nchi hiyo Lusaka. Maandamano hayo yamempa Hakainde Hichilema kiongozi wa chama cha Muungano kwa ajili ya Ustawi wa Taifa la Zambia fursa ya kunadi na kumtaka Rais Michael Sata wa nchi hiyo aingie naye kwenye uwanja wa mapambano ya kisiasa. Amesema katika mkusanyiko mkubwa wa wapinzani mjini Lusaka kuwa licha ya kuwepo vitisho vya kutiwa nguvuni viongozi wa upinzani wapinzani wataendelea kukosoa siasa za serikali. Kabla ya hapo Hichilema alikuwa ametiwa mbaroni na sasa licha ya kuachiliwa huru lakini bado anakabiliwa mahakamani na mashtaka ya kueneza propaganda za uongo dhidi ya Rais Sata. Maandamano hayo ni ya kwanza kuwahi kufanywa na wapinzani mjini Lusaka baada ya Michael Sata, ambaye ni mwanaharakati wa kisiasa wa zamani, kuchaguliwa kuwa rais wa nchi hiyo mwezi Septemba 2011.
Sata ambaye alianza harakati zake za kisiasa kwa kuteuliwa kuwa gavana wa Lusaka ni mwanachama wa chama tawala cha zamani cha Harakati ya Demokrasia ya Vyama Vingi MMD ambaye aliwahi kuhudumia nyadhifa mbalimbali katika baraza la mawaziri la nchi hiyo. Aliasisi Chama cha Taifa mwaka 2001 lakini hakufanikiwa kupata uongozi wa nchi hiyo katika chaguzi zilizofanyika mwaka 2006 na 2008. Katika uchaguzi uliofanyika mwaka 2011 alichuana na kumshinda Rupia Banda wa chama tawala. Ushindi huo ulimwezesha kuhudumia nafasi ya rais wa Zambia baada ya kushindwa mara nne katika chaguzi za kuwania nafasi hiyo huko nyuma. Ushindi wake kimsingi ulitokana na uungaji mkono mkubwa aliopata kutoka kwa wakaazi wa miji mikubwa. Alipata ushindi huo kupitia ahadi alizotoa kwenye kampeni zake za uchaguzi, za kuboresha maisha ya wananchi, kuandaa nafasi za ajira na kuimarisha viwango vya masomo kwa vijana. Licha ya hayo wapinzani wake walimtuhumu kuwa alifanya udanganyifu kwenye uchaguzi na kutekeleza siasa zinazipinga demokrasia. Inaonekana kuwa maandamano ya hivi karibuni mjini Lusaka ni ishara ya kwanza ya upinzani wa wazi wa wananchi dhidi ya serikali ya Sata. Kabla ya hapo, waungaji mkono wake pamoja na chama tawala walijaribu kuzuia maandaamano ya wapinzani mjini Lusaka lakini bila mafanikio. Askari usalama wameruhusu kufanyika maandamano hayo kwa kisingizio kwamba yatapunguza hasira za wananchi dhidi ya serikali.

No comments: