Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Sunday, February 8, 2015

Houthi: Baraza la mpito litajaza pengo la kisiasa Yemen

Kiongozi wa Harakati ya Ansarullah nchini Yemen amesema kuundwa Baraza la Taifa la Mpito ni hatua inayoweza kuvunja njama zote na kujaza pengo la kisiasa katika nchi hiyo ya Kiarabu.
Akizungumza katika kikao cha hadhara siku ya Jumamosi Abdul-Malik al-Houthi amesema kuna baadhi ya madola ya kigeni ambayo yamechochea kujiuzulu rais Abd Rabbu Mansur Hadi na waziri mkuu Khaled Bahah kwa lengo la kuibua pengo la kisiasa na kuvuruga taasisi za kiserikali.
Hatahivyo kiongozi huyo wa Harakati ya Ansarullah amesema watu wa Yemen wana azma ya kufikia malengo hayo halali. Aidha amesema mlango wa ushirikiano na umoja uko wazi kwa makundi yote ya kisiasa nchini humo.
Siku ya Ijumaa Harakati ya Ansarullah ilitangaza kuundwa  Baraza la Taifa la Mpito. Kwa mujibu wa tangazo hilo wanamapinduzi wa Ansarullah wamelivunja bunge na kutangaza uundwaji wa baraza la rais lenye wajumbe watano litakalofanya kazi kama serikali katika kipindi cha mpito cha miaka miwili. Tangazo hilo la katiba aidha limeongeza kuwa baraza la taifa la mpito lenye wajumbe 551 ambalo litachukua nafasi ya bunge litaundwa ili kuchagua baraza la rais katika jitihada za kumaliza mkwamo wa kisiasa ambao umekuwa ukishuhudiwa nchini Yemen.

No comments: