Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Thursday, June 12, 2014

US yaiomba Iran isaidie kutatua mgogoro wa Iraq

Marekani imeiomba Jamhuri ya Kiislamu ya Iran isaidie katika kutatua hali ya mambo nchini Iraq. Jen Psaki, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ameyasema hayo leo katika kikao na waandishi wa habari mjini Washington wakati akijibu swali la mwandishi mmoja wa habari kuhusiana na nafasi iliyonayo Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika kuisaidia Iraq kiulinzi dhidi ya wanamgambo wa kundi la kigaidi linalojiita Dola la Kiislamu la Iraq na Sham 'DAESH', ambapo amesema kuwa, anataraji kuiona Tehran ikisaidia kurejesha hali ya amani nchini Iraq.

Psaki anatoa matamshi hayo katika hali ambayo Waziri wa Mambo ya Nje wa Russia, Sergey Lavrov amesema kuwa kile kinachojiri nchini Iraq ni matokeo ya uingiliaji kijeshi wa Marekani na Uingereza katika nchi hiyo ya Kiarabu. Naye kwa upande wake Aleksey Pushkov, Mkuu wa Kamisheni ya Mambo ya Kimataifa katika bunge la Russia, amesema kuwa Marekani ni muhusika wa hali ya sasa nchini Iraq na mashambulizi yanayoendelea nchini humo. Pushkov amesema kuwa, uvamizi wa Marekani na Uingereza nchini Iraq miaka 10 iliyopita, ndio sababu iliyochangia makundi ya kigaidi kuweza kuudhibiti mkoa wa Mosul na maeneo mengine ya nchi hiyo.
Amesema kuwa, uvamizi wa Marekani kuanzia mwaka 2003 hadi 2011 nchini Iraq, ulitekelezwa kwa lengo la eti kupambana na makundi ya kigaidi, katika hali ambayo hii leo inashuhudiwa kuwa, matunda ya uvamizi huo ilikuwa ni kuzalisha zaidi makundi hayo ndani ya taifa hilo. Wakati huo huo, duru za habari nchini Iraq zinaeleza kuwa, wanamgambo wa Daesh wameanza kukimbia kutoka mjini Mosul kufuatia mashambulizi makali ya anga yanayofanywa na jeshi la nchi hiyo dhidi ya wanamgambo hao. Kwa mujibu wa habari, wapiganaji wa Daesh wameondoka katika barabara za mji huo na kukimbilia eneo la Rabia, kufuatia mashambulizi makali ya anga ya jeshi la Iraq.

No comments: