Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Sunday, June 1, 2014

Kutetereka maridhiano ya Kitaifa ya Wapalestina kutokana na kuyumba misimamo ya Mahmoud Abbas

Ismail Haniya, Waziri Mkuu wa serikali halali ya Palestina amesisitiza kuwa, tofauti zilizoko kati yake na Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina, Mahmoud Abbas, kamwe hazitovuruga makubaliano ya maridhiano ya kitaifa licha ya kuwa tofauti hizo hadi sasa zimechelewesha kuundwa serikali ya umoja wa kitaifa. Makubaliano hayo kati ya Fat'h na HAMAS yalisainiwa mwezi Aprili na moja ya vipengee muhimu ni kuundwa serikali ya umoja wa kitaifa itakayoyashirikisha makundi yote ya Palestina.

Licha ya Mahmoud Abbas kumteua Waziri Mkuu wake wa sasa, Rami Hamdallah, kuwa kiongozi wa serikali hiyo ya umoja wa kitaifa, bado kuna mambo mengi yanayokwamisha kutangazwa baraza jipya la mawaziri huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu na utawala haramu wa Israel. Wadhifa wa Waziri wa Mambo ya Nje ni moja kati ya mambo yanayoendelea kuzusha utata kati ya Fat'h na HAMAS na hivyo kuchelewesha uundwaji wa serikali mpya. Mahmoud Abbas anashinikiza kuteuliwa Riyadh al-Maliki kushikilia wadhifa huo lakini Hamas imepinga mashinikizo hayo. Pia Harakati ya HAMAS imepinga kuvunjwa Wizara ya Wafungwa ikisema hatua hiyo itatoa pigo kubwa la kisaikolojia kwa wafungwa wa Kipalestina wanaoendelea kuteseka kwenye jela za Wazayuni.
Wachambuzi wengi wanatiwa wasiwasi na kuendelea kujitokeza tofauti nyingi kati ya Fat'h na HAMAS na wanaitakidi kuwa suala hilo linayumbisha na kuhatarisha makubaliano ya maridhiano ya kitaifa ya Aprili 23.
Hapana shaka kwamba, kuungana na kushirikiana Wapalestina ndiyo njia pekee ya kukabiliana na njama za Wazayuni na waitifaki wao wa Magharibi wakiongozwa na Marekani. Kusimama pamoja Wapalestina kutawasaidia kudai na kupigania haki zao na uwezekano mkubwa ni kwamba watashinda kwenye mapambano hayo wakiwa kitu kimoja. Ni kutokana na kumaizi ukweli huo, ndio maana Wamarekani na Wazayuni wameanzisha fitna kubwa kujaribu kuyagonganisha vichwa makundi ya Wapalestina ili yasifikie lengo lao kuu la kuungana. Miongoni mwa njama za Wazayuni na Wamarekani ni kumtumia Mahmoud Abbas kwa kujaribu kumvuta tena kwenye mazungumzo na Wazayuni wakijidai kwamba wamekubali kulegeza kamba kwenye baadhi ya misimamo yao ya wali.
Kwa bahati mbaya, Mahmoud Abbas anaonekana kuchanganyikiwa na kuyumba kwenye misimamo yake licha ya kuahidi kwamba atafungamana na makubaliano ya maridhiano ya kitaifa ya mwezi Aprili. Baadhi ya weledi wa mambo wanaamini kuwa, huenda Abu Mazin anatumia kadhia ya umoja wa Wapalestina kama karata ya turufu kupima misimamo ya Wamarekani na Wazayuni na kuwalazimisha kulegeza kamba katika baadhi ya mambo. Wachambuzi hao wanasema si ajabu kwa Abbas kujiondoa kenye makubaliano na HAMAS na kurudi tena kwenye meza ya mazungumzo eti ya amani na Wazayuni iwapo ataona maslahi yake yanadhaminiwa na kulindwa kwa njia hiyo. Hatua ya Abbas ya kumteua Riyadh al-Maliki ambaye tangu mwanzoni ana matatizo na wanachama wa HAMAS ni miongoni mwa harakati za kiongozi huyo za kuchafua anga ya maridhiano kati ya makundi ya Kipalestina.
Alaa kulli hali, kuyumba misimamo ya Mahmoud Abbas mkabala wa maridhiano ya kitaifa kumekosolewa na Wapalestina wengi wanaohofia kwamba fursa iliyojitokeza ya kuungana yumkini ikapotea tena na hivyo kuwapa nguvu Wazayuni kushadidisha hujuma, jinai na dhulma zao za kila siku dhidi yao.

No comments: