Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, May 17, 2014

Machafuko yaendelea Jamhuri ya Afrika ya Kati

Jamhuri ya Afrika ya Kati imeendelea kukumbwa na machafuko ambapo kwa uchache watu watatu wameripotiwa kuuawa katika machafuko hapo jana. Habari kutoka nchini humo zinasema kuwa, watu wenye silaha wamefanya mashambulio katika vijiji kadhaa vya kaskazini magharibi mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati. Aidha mashambulio hayo yaliambatana na wizi na uporaji wa mali za wanavijiji.
Wanavijiji hao wameziambia duru za habari kwamba, vikosi vya Umoja wa Afrika vilivyoko nchini humo MISCA havionyeshi radiamali yoyote kuhusiana na mashambulio hayo.  Hivi karibuni pia, Rais Catherine Samba-Panza wa Jamhuri ya Afrika ya Kati alivikosoa vikali vikosi vya kigeni vilivyoko nchini humo kutokana na kushindwa kwao kuyapokonya silaha makundi ya wanamgambo yanayobeba silaha.  Machafuko katika Jamhuri ya Afrika ya Kati yanaendelea huku Waislamu wa nchi hiyo wakiwa ndio wahanga wakuu wa machafuko hayo, kutokana na kuuawa na wanamgambo wa Kikristo wa Anti-Balaka. Tokea mgogoro wa Jamhuri ya Afrika ya Kati uanze mwezi Disemba mwaka uliopita, Waislamu wapatao laki tatu na sitini elfu wa nchi hiyo wamekimbilia katika nchi jirani zikiwemo za Cameroon na Chad.

No comments: