Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Tuesday, May 20, 2014

Kusonga mbele wanamgambo hadi mji mkuu wa Libya, Tripoli

Mapigano makali yanaendelea kushuhudiwa nchini Libya huku wanamgambo watiifu kwa Khalifa Haftar, jenerali mstaafu na kamanda wa zamani wa jeshi la nchi kavu nchini humo wakisonga mbele hadi Tripoli, mji mkuu wa Libya. Mashambulio ya makombora na mizinga ya wanamgambo wanaobeba silaha kwenye makao ya Kongresi ya Taifa ya Libya yaani bunge yanaonyesha kuwa, Libya imetumbukia kwenye lindi la ukosevu wa amani. Duru za kisiasa zinasema kuwa, kile kinachojitokeza nchini Libya ni mithili ya mapinduzi.
Kongresi ya Taifa ya Libya, chombo pekee cha kutunga sheria nchini humo imesimamisha shughuli zake na hii ni katika hali ambayo wanamgambo pia wameshambulia majengo ya televisheni mjini Tripoli. Mapigano kati ya vikosi vya serikali na wanamgambo watiifu kwa Jenerali mstaafu Khalifa Haftar yangali bado yanaendelea mjini Tripoli. Salah al Marghani Waziri wa Sheria wa Libya ametangaza kuwa, karibu watu 60 wameuawa na kujeruhiwa kwenye mapigano yaliyotokea jana mjini Tripoli. Duru za habari zinasema kuwa, maeneo ya kiistratijia ya Libya yamekuwa yakilengwa na mashambulizi ya wanamgambo hao. Dalili zote zinaonyesha kwamba wanamgambo wanafanya juhudi za kutaka kupora madaraka kwa nguvu nchini humo. Swali linalojitokeza hapa ni hili kwamba, je senario ya Misri inaweza kukaririwa nchini Libya? Nchini Libya, wanajeshi waliopata mafunzo ya kijeshi wakati wa utawala wa Kanali Muammar Gaddafi, hivi sasa ndio wanaoendesha harakati za kijeshi dhidi ya serikali ya mpito na hata kufika Tripoli wakitokea mji wa Benghazi ulioko mashariki mwa nchi hiyo. Hatua ya wanamgambo hao ya kulilazimisha bunge kufunga shughuli zake, ni mwanzo wa kutatiza shughuli za uendeshaji wa serikali ya Libya. Inaonekana kuwa, wanajeshi wa zamani wanataka kuzusha ghasia na machafuko ili waweze kufikia malengo yao. Jenerali mstaafu Khalifa Haftar na wanamgambo watiifu kwake wanaelewa vyema kwamba, Libya haina jeshi imara na lenye nguvu. Hivi sasa nchi hiyo imegawanyika katika makundi mbalimbali yakiwemo ya wanamgambo, wanamapinduzi wa zamani na makumi ya makundi mengine ya kisiasa, kikabila na ya kijeshi na kila kundi limejizatiti na kudhibiti baadhi ya maeneo nchini humo. Sababu hiyohiyo ndiyo iliyopelekea Jenerali mstaafu Haftar na wafuasi wake watiifu kutunisha misuli yao dhidi ya majeshi ya serikali. Hali inayotawala hivi sasa nchini Libya inaonyesha kuwa, kundi lolote litakaloweza kutoa pigo dhidi ya mji mkuu wa nchi hiyo linatarajiwa kushika hatamu za uongozi katika siku zijazo. Imeelezwa kuwa Jenerali huyo mstaafu amekuwa na nguvu zaidi za kijeshi kutokana na uwezo wake wa kuzidhibiti kambi zote za kijeshi na kiusalama katika eneo lenye utajiri mkubwa wa mafuta lililoko mashariki mwa nchi hiyo. Jenerali mstaafu Haftar anafanya juhudi za kushambulia maeneo muhimu na nyeti, ili aweze kuidhoofisha serikali na hatimaye kuchukua hatamu za uongozi. Baadhi ya duru za kisiasa zinaamini kwamba, wanajeshi wastaafu wa utawala wa Gaddafi wanapanga mikakati ya kurejea kwenye uwanja wa kisiasa nchini humo. Iwapo hali hiyo itathibiti, bila shaka hali ya kisiasa ya Libya itafanana na ile ya Misri, na bila shaka nchi za Magharibi ndizo zitakazonufaika na hali hiyo. Uzoefu unaonyesha kuwa, nchi za Magharibi zinaweza kuwa bega kwa bega na wanajeshi.  Inavyoonekana ni kuwa, hali inayoshuhudiwa hivi sasa katika nchi za Misri na Libya, ni kwa wanajeshi kuwa katika mikakati ya kuchukua madaraka.  Kwa vile Libya inakabiliwa na machafuko kama ilivyokuwa Misri, hakuna shaka kuwa nchi hiyo kwa mara nyingine tena itakabiliwa na hatima ya kuingiliwa na Marekani na madola ya Magharibi katika harakati za kisiasa za nchi hiyo. Bila shaka nchi hizo zinaingilia mambo ya ndani ya nchi nyingine kwa lengo la kudhamini maslahi yao haramu barani Afrika, kwa kupora maliasili na utajiri wa mafuta. Hivi karibuni, Rais Barack Obama wa Marekani alitahadharisha kwamba, iwapo Libya itashindwa kurejesha amani na utulivu, nchi hiyo pamoja na wanachama wengine wa NATO wataingilia mgogoro wa nchi hiyo iliyoko kaskazini mwa Afrika kwa lengo la kuongoza mwenendo wa kisiasa wa nchi hiyo. 

No comments: