Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, July 6, 2013

Jumamosi, Julai 6 2013

Leo ni Jumamosi tarehe 27 Shaaban mwaka 1434 Hijiria sawa na tarehe 6 Julai mwaka 2013 Miladia.
Siku kama ya leo miaka 49 iliyopita, nchi ya Kiafrika ya Malawi ilipata uhuru toka kwa Muingereza. Kabla ya uhuru ardhi hiyo ilikuwa ikijulikana kwa jina la Nyasaland. Mwaka 1859, kundi wamisionari kutoka Uskochi likiwa na mvumbuzi mashuhuri David Livingstone liliwasili nchini Malawi. Mwaka 1891 Waingereza waliidhibiti nchi hiyo na kuiweka chini ya himaya yao. Aidha mwaka 1953, Uingereza ikiwa na lengo la kuanzisha umoja baina ya ardhi zilizokuwa chini ya udhibiti wake, ilianzisha Shirikisho la Rhodesia na Nyasaland.
Ilikuwa mwaka 1962 wakati kuliposhuhudiwa upinzani na maandamano makubwa ya kutaka kuvunjwa shirikisho hilo. Hatimaye mwaka 1963 shirikisho hilo lilisambaratika na mwaka uliofuata Nyasaland ikajipatia uhuru na kuitwa Malawi.

Miaka 38 iliyopita na katika siku kama ya leo, visiwa vya Comoro vilivyoko barani Afrika vilipata uhuru. Karne kadhaa zilizopita kabla ya hapo, visiwa hivyo vilivamiwa na kudhibitiwa na Waarabu. Ni katika kipindi hicho ndipo wananchi wengi wa Comoro waliposilimu na kuingia katika dini tukufu ya Kislamu. Kuanzia karne ya  16, kwa muda fulani visiwa hivyo vilikaliwa kwa mabavu na Wareno, na mwaka 1842 sehemu ya visiwa hivyo ikadhibitiwa na Ufaransa na taratibu ardhi yote ya Comoro ikawa chini ya udhibiti wa mkoloni huyo. Baada ya mapambano ya miaka kadhaa ya kupigania uhuru, hatimaye katika siku kama ya leo mnamo mwaka 1975, visiwa vya Comoro vilijikomboa na kupata huru.

Na siku kama ya leo miaka 51iliyopita aliaga dunia mwandishi wa Kimarekani kwa jina la Faulkner William. Alizaliwa mwaka 1897. Faulkner alirejea nchini kwake baada ya kushiriki katika Vita vya Kwanza vya Dunia. Mwandishi William alianza kuandika hadithi mwaka 1925 baada ya kufahamiana na Sherwood Anderson mwandishi mwenzie wa Kimarekani. Katika hadithi zake Faulkner alikuwa akibainisha hali mbaya ya kijamii huko Marekani hususan ubaguzi wa rangi uliokuwa ukiwakabili raia weusi wa nchi hiyo. Riwaya za mwandishi huyo zimekuwa na taathira kubwa katika sekta ya uandishi wa leo nchini Marekani.

No comments: