Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, July 8, 2013

Al-Baradei akataa pendekezo la uwaziri mkuu Misri

Kiongozi wa upinzani nchini Misri Mohamed al Baradei, amekataa pendekezo la kuwa waziri mkuu wa serikali ya mpito ya nchi hiyo. Mbali na kukataa pendekezo hilo, Al-Baradei amependekeza wadhifa huo uchukuliwe na Ziyad Bahaud-Din. Aidha kiongozi huyo wa upinzani, ametaka kuchukua wadhifa wa naibu wa waziri mkuu katika masuala ya kisiasa. Hayo yanajiri katika hali ambayo waungaji mkono wa Harakati ya Ikhwanul Muslimin na Rais aliyeenguliwa madarakani, Muhammad Mursi, wameendelea kufanya maandamano mashariki mwa mji mkuu wa nchi hiyo, Cairo na kutaka rais huyo arejeshwe madarakani.
Mbali na hayo, waandamanaji pia wametaka aachiliwe huru yeye na baadhi ya viongozi wa Ikhwanul Muslimin wanaoshikiliwa na jeshi la nchi hiyo. Wakati huo huo jeshi la Misri limeweka doria kali katika kila kona kwa lengo la kurejesha hali ya usalama nchini. Jana Rais Vladimir Putin wa Russia alionya juu ya hatari ya machafuko yanayoendelea nchini Misri kuwa yanaweza kuitumbukiza nchi hiyo kwenye mapigano ya wenyewe kwa wenyewe. Rais Vladimir Putin amesema tayari Syria imetumbukia vya kutosha katika vita vya ndani na kuwa jambo la kusikitisha ni kuona hatari ya kutumbukia Misri katika mgogoro kama huo.

No comments: