Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, June 19, 2013

Sita wafa ajalini Bukoba, Mbunge ‘Sugu’anusurika

Kagera. Watu sita wamefariki dunia wilayani Muleba mkoani Kagera baada ya basi la abiria kupinduka katika ajali inayodaiwa kuwa ni uzembe wa dereva ambaye alikuwa katika mwendo kasi huku akiongea na simu ya kiganjani.
Ajali hiyo imetokea jana mchana katika mteremko wa Kalonga Tarafa ya Kimwani wakati basi hilo likitokea Bukoba kwenda Geita. Dereva wa gari hilo alifariki papo hapo katika ajali hiyo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera,Philip Kalangi alipotafutwa kutoa ufafanuzi wa ajali hiyo alisema atafutwe baadaye kwani alikuwa anaelekea eneo la ajali.
Mkuu wa Wilaya ya Muleba, Lembres Kipuyo alisema taarifa za awali zinaonyesha kuwa dereva wa basi hilo alikuwa katika mwendo kasi huku akiongea na simu na kuwa miongoni mwa abiria sita waliofariki akiwamo mama na mtoto wake.
Wakati huohuo, Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ amenusurika kifo baada ya gari lake kupata ajali maeneo ya Katesh wakati akitoka Mbeya kwenda Arusha kushiriki mazishi ya wafuasi wa Chadema waliofariki kwa mlipuko wa bomu.
Akizungumza kwa simu kutoka Kituo cha Polisi Katesh, mbunge huyo alisema hakuna aliyekufa katika ajali hiyo iliyohusisha gari lake na basi la Best Line linalofanya safari zake kati ya Mwanza na Moshi.
Mashuhuda wa ajali hiyo walisema, gari la mbunge huyo liliharibika upande wa kushoto alikokuwa amekaa kiongozi huyo mwenye mvuto kwa vijana nchini.
Gari hilo aina ya Landcruiser lilikuwa likitokea Mbeya wakati basi hilo la abiria likitokea Mwanza -kwenda Moshi huku wakifuatana na kwa mujibu wa mashuhuda walipofika katika kona ya maeneo ya Katesh kituoni , basi hilo lilikunja kona kuingia kituoni na ndipo lilipogongana na gari la mbunge huyo wa Mbeya mjini kwa tiketi ya Chadema.
Kamanda wa Polisi mkoani Manyara, Akili Mpwapwa amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kuongeza kuwa uchunguzi bado unaendelea.
Sugu alikuwa akiwahi mazishi ya walifariki kwa bomu mjini Arusha, lililotokea Jumapili na kuua watu na kujeruhi wengine 36.

No comments: