Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, June 22, 2013

Jumamosi, Juni 22, 2013

Leo ni Jumamosi tarehe 13 Shaaban mwaka 1434 Hijiria, inayosadifiana na tarehe 22 Juni mwaka 2013 Miladia.
Siku kama ya leo miaka 234 iliyopita, alifariki dunia Hussein bin Muhammad Swaleh Khalidi, mwanazuoni mkubwa wa karne ya 13 Hijiria. Alizaliwa huko Baitul Muqaddas na akiwa katika mji huo alianza kujifunza elimu mbalimbali za zama hizo. Khalidi alikuwa mwanazuoni mwenye basira, mwandishi aliyetabahari na pia alisifika kwa hati nzuri. Hassan bin Muhammad Saleh Khalidi vilevile alikuwa na kipaji cha kusoma vizuri mashairi hasa ya Kiarabu. Mwanazuoni huyo ameacha vitabu kadhaa.

Miaka 32 iliyopita sawa na tarehe Mosi Tir mwaka 1360 kwa mujibu wa Kalenda ya Kiirani, hayati Imam Ruhullah Khomeini alipasisha uamuzi wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu wa kutokuwa na imani na rais wa wakati huo Abul Hassan Bani Sadr na kwa utaratibu huo kiongozi huyo akalazimika kung'atuka madarakani. Bani Sadr ni miongoni mwa watu waliojidhihirisha kuwa wapenzi na watetezi wa harakati za Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran baada ya Imam Khomeini kuhamia Paris, Ufaransa na alifanikiwa kushika madaraka ya nchi na kuwa rais katika uchaguzi wa kwanza wa baada ya Mapinduzi ya Kiislamu nchini kwa kutumia ujanja wa kipropaganda. Muda mfupi baadaye Imam Khomeini alimkabidhi ukamanda wa majeshi ya Jamhuri ya Kiislamu. Hata hivyo Bani Sadr aliyekuwa mtu mwenye uchu wa madaraka, mwenye kiburi na msaliti alianza mara moja kushirikiana na makundi yaliyokuwa yakipinga Mapinduzi ya Kiislamu kwa lengo la kuangusha utawala wa Kiislamu nchini Iran.
Na miaka 380 iliyopita mnajimu, mtaalamu wa hisabati na mwanafizikia wa Italia Galileo Galilei alilazimika kukana itikadi zake za kisayansi na kielimu mbele ya viongozi wa Kanisa. Mwaka 1632 Galilei aliandika kitabu akijibu na kukosoa mitazamo ya Betlemosi kuhusu sayari ya jua na kutangaza kuwa dunia inazunguma jua. Mwaka mmoja baadaye Papa wa Kanisa Katoliki alimwita Galileo mjini Roma na kuitaja mitazamo hiyo ya kisayansi kuwa ukafiri. Kwa msingi huo, kanisa lilimlazimisha Galileo akane itikadi zake za kielimu la sivyo akabiliwe na adhabu ya kifo. Japokuwa msomi huyo alikana mitazamo yake hiyo ya kielimu kidhahiri tu lakini wakati alipotoka nje ya mahakama alipiga chini mguu wake na kuiambia ardhi: "Licha ya haya yote lakini wewe unazunguka."

No comments: