Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, June 29, 2013

Hali ya mambo nchini Misri yazidi kuharibika

Hali ya mambo nchini Misri inaendelea kuharibika na inaonekana viongozi wa nchi hiyo wanajiandaa kukabiliana na hali yoyote inayoweza kutokea kutokana na kuongezeka malalamiko ya wananchi. Katika siku za hivi karibuni Medani ya Tahrir kwa mara nyingine tena imekuwa uwanja wa malalamiko ya wapinzani wa serikali ya Rais Muhammad Mursi wa nchi hiyo. Kama ilivyokuwa wakati wa maandamano ya kupinga utawala wa dikteta Husni Mubarack, wapinzani wa Mursi nao pia wamekuwa wakikesha kwenye uwanja huo na kupiga nara za kupinga serikali yake.
Ripoti zinasema mapigano yametokea kati ya askari usalama na wapinzani wa Mursi katika mikoa mingine mitatu ya Dakahlia, Sharqiya na Gharbiya ambapo watu wawili wameuawa na wengine 300 kujeruhiwa. Malalamiko na ghasia hizo zinaripotiwa katika hali ambayo hivi karibuni Rais Mursi aliadhimisha mwake wake wa kwanza tokea aingie madarakani ambapo alikiri kwamba kuna baadhi ya makosa yaliyofanyika katika serikali yake katika kipindi hiki na kuahidi kuyarekebisha. Wakati huohuo amependekeza kufanyike mazungumzo ya kitaifa ili kuiondoa nchi hiyo kwenye mgogoro uliopo wa kisiasa. Amependekeza kubuniwa kamati ambayo itajumuisha wawakilishi wa vyama na makundi yote ya kisiasa na kisha kujadili na kuwasilisha mapendekezo ya kutatuliwa matatizo hayo, jambo ambalo limepingwa vikali na mrengo wa upinzani. Akizungumzia suala hilo, Ahmad Bahau Deen Sha'ban, mratibu wa Jumuiya ya Kitaifa ya Mabadiliko ya Misri amesema kwamba pendekezo la Rais Mursi la kubuniwa kamati ya kufuatilia na kutatua makosa yaliyofanywa na serikali yake halina nia nzuri bali ni la kimeonyesha tu na lisilokuwa na maana yoyote. Amesema pendekezo kama hilo liliwahi kutolewa huko nyuma lakini halikufanyiwa kazi. Khalid Dawoud, Msemaji wa Harakati ya Wokovu wa Kitaifa pia amekosoa matamshi hayo ya Mursi na kuyataja kuwa yasiyo na tofauti yoyote na matamshi kama hayo aliyotoa huko nyuma. Wapinzani wanasema kwamba matamshi ya hivi karibuni ya Rais Mursi hayana kitu chochote kipya na kwamba hatua yake ya kuwataka wapinzani anaowaita kuwa ni maadui wa demokrasia, washiriki kwenye mazungumzo ya umoja wa kitaifa, imepitwa na wakati. Misimamo hiyo ya pande mbili hasimu inachukuliwa katika hali ambayo wapinzani wanasisitiza kwamba wameazimia kufanya maandamano ya kuadhimisha mwaka mmoja wa mapinduzi ya Wamisri hapo siku ya Jumapili Juni 30. Aiman Nur, mkuu wa Chama cha Ghad at-Thaura amesema kuwa amesikitishwa na matamshi ya hivi karibuni ya Mursi na kusisitiza kuwa chama chake kitashiriki katika maandamano hayo. Chama cha Wokovu wa Kitaifa ambacho ndicho chama kikubwa zaidi cha upinzani nchini Misri kimewataka wananchi wote wa nchi hiyo washiriki kwenye maandamano hayo. Wito huo unatolewa katika hali ambayo jeshi la nchi hiyo limetoa taarifa likisema kuwa usalama wa nchi hiyo uko hatarini na kwamba liko tayari kuchukua hatua ya kuulinda. Kwa kuzingatia hali hiyo wataalamu wa mambo wanasema kwamba fursa ya kulinda mapinduzi ya Misri, inaendelea kutoweka kwa kasi.

No comments: