Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Thursday, January 24, 2013

Matokeo ya uchaguzi wa kabla ya wakati wa bunge la utawala wa Kizayuni

Matokeo ya awali ya uchaguzi wa kabla ya wakati wa bunge la utawala wa Kizayuni wa Israel yanaonyesha kuwa awamu nyengine mpya ya mtikisiko na mvutano wa kisiasa na mizozano baina ya vyama inaujongelea utawala huo haramu. Ripoti tofauti zinaonyesha kuwa chama cha Benjamin Nentanyahu cha Likud kimeshindwa kupata ushindi mutlaki katika uchaguzi huo. Matokeo ya awali ya uchaguzi wa bunge la Israel yanaonyesha kuwa chama cha Likud kimepata ushindi mdogo dhidi ya wapinzani wake. Sambamba na hayo chama kiitwacho Yisrael Beitenu "Israel Nyumba Yetu" kinachoongozwa na Avigdor Lieberman na ambacho kilikuwa muitifaki wa Likud katika uchaguzi huo nacho pia kimeshindwa kupata kura za maana, hali ambayo inayumbisha nafasi ya muungano wa vyama hivyo viwili katika uga wa kisiasa wa utawala wa Kizayuni.
Matokeo ya awali ya uchaguzi wa bunge la utawala wa Kizayuni yanaashiria kuvurugika mahisabu ya kisiasa aliyokuwa amepiga Netanyahu ya kuweza kujiimarisha zaidi kimadaraka kupitia uchaguzi alioupigia upatu wa kabla ya wakati wa bunge la utawala wa Kizayuni wa Israel. Matukio na mabadiliko ya kisiasa yanayojiri ndani ya utawala wa Kizayuni yanaonyesha kuwa kutokana na kura zilizopigwa kuna uwezekano mkubwa kwamba Shimon Peres, Rais wa utawala huo ghasibu atampa kiongozi wa chama cha Likud Benjamin Netanyahu jukumu la kuunda serikali mpya, hata hivyo kibarua kigumu mno kitamkabili Nentanyahu hata kuweza kuifanikisha kazi hiyo. Kwa kuwa hakuweza kupata ushindi wa kishindo alioutarajia, Netanyahu atalazimika kuunda serikali ya muungano mkubwa wa vyama vyenye mielekeo tofauti ya mirengo ya kulia na kushoto suala ambalo litazidi kuufanya uthabiti wa serikali hiyo uwe tete na wa kulegalega. Ikiwa Netanyahu atashindwa kuunda serikali kulingana na muda uliowekwa, Peres atakipa chama kingine jukumu la kuitekeleza kazi hiyo. Na hivyo ndivyo ilivyotokea pia katika uchaguzi uliopita wa bunge la 18 la utawala wa Kizayuni ambapo licha ya chama cha Kadima kupata kura nyingi kilishindwa kuunda serikali kwa wakati uliopangwa na matokeo yake ni kwamba chama cha Likud kinachoongozwa na Netanyahu ndicho kilichounda serikali mpya licha ya kupata kura chache kulinganisha na Kadima katika uchaguzi huo.
Alaa kulli hal matokeo ya uchaguzi wa kabla ya wakati wa bunge la utawala wa Kizayuni sio tu yameigeuza kuwa jinamizi njozi aliyokuwa nayo Benjamin Netanyahu ya kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi huo lakini pia yanadhihirisha wazi kwamba utawala huo bandia sasa unaelekea kwenye awamu mpya ya mtikisiko na hali ya mchafukoge wa kisiasa. Katika hali kama hiyo haitaokuwa ajabu kwa serikali ijayo ya utawala wa Kizayuni nayo pia kama aghalabu ya serikali zilizotangulia ikashindwa kukamilisha kipindi cha miaka minne madarakani na kulazimika kuitisha uchaguzi mwengine wa kabla ya wakati. Chaguzi za mara kwa mara za kabla ya wakati katika utawala wa Kizayuni zinazidi kuonyesha kuwa giza totoro na wingu zito limegubika anga ya mustakabali wa kisiasa wa utawala huo haramu. Mtikisiko wa kisiasa ndani ya utawala wa Kizayuni unaochanganyika na mazonge mengine ya ndani yakiwemo ya kiuchumi na kijamii yanazidi kuizamisha Israel kwenye lindi la mgogoro na kuongeza kasi ya mchakato wa kuporomoka na kusambaratika utawala huo haramu.../

No comments: