Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Tuesday, June 3, 2014

Wito wa maridhiano ya kitaifa nchini Sudan Kusini

Huku makundi hasimu ya Sudan Kusini yakijiandaa kwa duru mpya ya mazungumzo ya amani mjini Addis Ababa, Ethiopia, Rais Salva Kiir Mayardit ametoa wito wa kufanyika maridhiano ya kitaifa ili kuinusuru nchi hiyo changa zaidi barani Afrika. Akilihutubia bunge la taifa, Rais wa Sudan Kusini amesema pana haja ya pande zote hasimu kusameheana na kushikana pamoja ili kuijenga nchi. Amewataka wananchi wote kuisaidia serikali yake kudumisha umoja wa kitaifa. "Sina kinyongo wala hasira dhidi ya mtu yeyote hata wale ambao hatuafikiani katika masuala kadhaa. Tunaweza kuketi na kujadiliana masuala yaliyopo na hatimaye kutatua tofauti zetu kwa maslahi ya taifa" amesema Rais Kiir ambele ya wabunge wa nchi yake.

Mwito wa rais Salva Kiir unakuja siku chache  baada ya Riek Machar, kiongozi wa waasi na makamu wa zamani wa rais wa Sudan Kusini kusema kuwa yuko tayari kushiriki kwenye mchakato wa maridhiano ya kitaifa kwa lengo la kuzuia umwagikaji zaidi wa damu nchini mwake. Dkt Machar amenukuliwa akisema, uwezekano upo kwa yeye kusaini makubaliano ya kudumu ya amani kati yake na Rais Salva Kiir. Hii ni katika hali ambayo, Jumatano ya hapo kesho Juni 4 kunatarajiwa kufanyika duru nyingine ya mazungumzo kati ya wajumbe wa serikali ya Juba na wale wanaomuunga mkono Dk. Riek Machar huko Addis Ababa, Ethiopia. Mazungumzo hayo yamekuwa yakisimamiwa na Jumuiya ya Kieneo ya IGAD ambapo mwezi uliopita wa Mei, kwa mara ya kwanza tangu kuzuka machafuko Sudan Kusini, Rais Salva Kiir alikutana ana kwa ana na hasimu wake Dk. Machar na kusaini makubaliano ya usitishwaji vita. Hata hivyo makubaliano hayo yalikiukwa saa chache tu baada ya kusainiwa, huku kila upande ukiunyooshea kidole cha lawama upande wa pili na kusema ndio uliokiuka makubaliano hayo. Licha ya hayo yote, Rais Salva Kiir amesema, ujumbe wa serikali yake utakwenda Addis Ababa ukiwa na nia njema na irada thabiti ya kuutafutia ufumbuzi mgogoro wa Sudan Kusini.
Ingawa kuna kauli za kutia matumaini kutoka kwa viongozi wa pande zote hasimu katika mgogoro wa Sudan Kusini, lakini hali halisi ya mambo ni kinyume kabisa na kauli hizo. Umoja wa Mataifa umetahadharisha kuwa, kuna hatari ya kuzuka hali mbaya ya kibinadamu Sudan Kusini iwapo mapigano hayatasitishwa. Hii ni katika hali ambayo, ripoti zinaonyesha kuwa mgogoro huo umeendelea kushika kasi katika siku za hivi karibuni na kwamba raia zaidi wanaendelea kukimbia makazi yao. Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa wiki iliyopita lilipitisha azimio linalotaka kurejeshwa amani na utulivu haraka iwezekanavyo huko Sudan Kusini.
Takwimu zinaonyesha kuwa, tangu kuzuka mapigano Disemba 15 mwaka uliopita, zaidi ya wakimbizi 300,000 kutoka Sudan Kusini wamekimbilia katika nchi za Ethiopia, Kenya, Sudan na Uganda.
Taasisi mbalimbali za kutetea haki za binadamu ikiwemo Kamisheni Kuu ya kutetea haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa zimekemea ukiukwaji wa haki za binadamu na jinai za kivita zilizotendwa na pande zote husika kwenye mgogoro wa Sudan Kusini.
Wachambuzi wengi wanafuatilia kwa karibu duru mpya ya mazungumzo kati ya serikali ya Juba na upande wa Riek Machar yanayotarajiwa kuanza kesho nchini Ethiopia, ili kuona kama kauli za matumaini walizotoa mahasimu hao wa kisiasa zitaambatana na vitendo kwa lengo la kukomesha kabisa mapigano Sudan Kusini.

No comments: