Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, June 2, 2014

Waasi wa Anti-Balaka Jamhuri ya Afrika ya Kati waharibu msikiti

Huku machafuko yakizidi kushika kasi nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, kwa mara nyingine tena, waasi wa Kikristo wa Anti-Balaka wamevamia msikiti mmoja mjini Bangui na kuuharibu kabisa. Hii ni katika hali ambayo hivi karibuni pia kanisa moja mjini humo lilishambuliwa na watu wenye silaha wanaosadikiwa kuwa na mafungamano na waasi hao na kufanya mauaji dhidi ya watu wasiopungua 30 akiwemo padri wa kanisa hilo. Kufuatia kuongezeka wimbi la vitendo vya ukatili nchini humo, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, sambamba na kutoa tamko kuhusiana na suala hilo, limeyataka makundi yanayohusika katika vitendo hivyo, kuweka chini silaha na kufuata mkondo wa amani nchini humo.

Katika ripoti hiyo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeitaka serikali ya Rais Catherine Samba-Panza wa Jamhuri ya Afrika ya kati, kuwachukulia hatua kali na za haraka wahusika wa vitendo hivyo. Vile vile Msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR amelaani shambulizi hilo dhidi ya kanisa mjini Bangui, na kuyataja machafuko hayo ya hivi karibuni kuwa ni dalili za kuzorota hali ya usalama nchini humo. Adrian Edwards amelaani mashambulizi dhidi ya maeneo ya ibada ambayo ndio maeneo yaliyosalia kwa ajili ya kuwahifadhi wakimbizi na kutaka kukomeshwa mashambulizi hayo mara moja. Hayo yanajiri katika hali ambayo, wakazi wa mjini Bangui, wamefanya maandamano makubwa mjini humo wakimtaka Rais Panza ajiuzulu kutokana na kile wanachodai kuwa ni kushindwa serikali yake ya mpito kumaliza machafuko nchini mwao.
Kwa upande mwingine baada ya kushambuliwa kanisa mjini Bangui, Rais Catherine Samba-Panza aliwahutubia wananchi na kulaani vikali tukio hilo aliloliita kuwa la kigaidi. Aidha alionyesha kusikitishwa kwake na ongezeko la vitendo vya ukatili mjini Bangui na kuenea vitendo hivyo katika maeneo mengine ya nchi hiyo. Amesema jambo hilo linatishia usalama wa taifa zima. Hata hivyo kile kinachowashangaza wengi ni radiamali ya vyombo vya habari vya nchi za Magharibi na kujaribu kwao kufunika ukweli wa matukio ya hivi karibuni nchini humo. Hii ni katika hali ambayo shambulizi dhidi ya kanisa hilo limeakisiwa kwa upana mno katika vyombo vya habari vya Magharibi, huku shambulizi dhidi ya msikiti likiwa limepuuzwa kabisa.
Kabla ya hapo pia Waislamu wengi waliuawa na kujeruhiwa katika mashambulizi ya waasi hao wa Kikristo wa Anti-Balaka katika misikiti kadhaa nchini humo. Waasi hao walianzisha mashambulizi yao ya kidini dhidi ya Waislamu tangu mwezi Disemba mwaka jana. Ripoti zinasema kuwa, tangu kuanza machafuko hayo ya ndani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, zaidi ya watu milioni moja yaani karibu robo nzima ya wananchi wa nchi hiyo ya katikati mwa Afrika, wamekuwa wakimbizi ndani na nje ya nchi. Kabla ya hapo pia na kufuatia kushadidi mapigano ya kikaumu na kuongezeka machafuko nchini humo, viongozi wa Kiislamu na wale wa Kikristo walitangaza umoja kati ya wafuasi wa dini hizo. Hata hivyo juhudi hizo hazikuweza kupunguza machafuko nchini humo. Kwa upande mwingine, mapigano ya kikaumu nchini humo yanajiri mbele ya macho ya maelfu ya askari wa kimataifa wa kulinda amani wakiwemo wale wa Ufaransa. Kuwepo askari hao nchini humo, hakujasaidia lolote katika kuzuia mauaji ambayo Waislamu ndio wahanga wake wakuu wa machafuko hayo.

No comments: