Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Thursday, June 12, 2014

Mkutano wa kimataifa wa kukabiliana na vitendo vya ubakaji wakati wa vita

Jiji la London, Uingereza ni mwenyeji wa mkutano wa kimataifa unaojadili vitendo vya ubakaji vinavyotokea vitani katika maeneo mbalimbali duniani. Mkutano huo wa kimataifa umeanza shughuli zake leo na kuhudhuriwa na wawakilishi kutoka nchi 117. Taarifa zinasema kuwa, imetolewa protokali ya kimataifa kwenye mkutano huo yenye lengo la kuchunguzwa jinai na ubakaji wakati wa vita na kufuatiliwa kisheria watenda jinai hizo.

Phumzile Mlambo-Ngcuka Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia masuala ya wanawake amesema kuwa, ijapokuwa wanaume hubakwa kwenye maeneo ya vita, lakini wanawake ndiyo wahanga wakubwa zaidi wa jinai hizo kwani karibu asilimia 70 ya wanawake huwa walengwa wakuu wa vitendo hivyo vya ubakaji wakati vinapotokea vita katika maeneo mbalimbali duniani. Washiriki wa mkutano huo wameonyesha matumaini ya kupatikana njia zitakazoweza kukabiliana na vitendo hivyo vichafu, na kutekelezwa haki na usawa kwa wahanga wa vitendo hivyo.
Katika miaka ya hivi karibuni, wanawake katika nchi za Bosnia Herzegovina, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Somalia walikuwa waathirika wakubwa wa vitendo vya ubakaji na udhalilishaji wa kijinsia. Nchini Bosnia Herzegovina ambapo wanawake wasiopungua elfu hamsini walibakwa wakati wa vita, na watendaji wa jinai hizo bado hawajachukuliwa hatua zozote za kisheria licha ya kupita miongo miwili sasa. Vitendo vya ubakaji dhidi ya wanawake wakati wa vita siyo jambo jipya katika zama hizi, lakini kasi ya vitendo hivyo vichafu inazidi kutia wasiwasi mno. Jambo la kusikitisha ni kwamba vitendo hivyo vichafu vinaonekana kuwa jambo la kawaida, na hadi sasa hakuna mikakati yoyote ya maana iliyowekwa kukabiliana na vitendo hivyo au hatua zinazopaswa kuchukuliwa dhidi ya watenda jinai hizo.
Alaa kulli haal, wanawake ndiyo waathirika wakubwa wa vitendo vya ubakaji ikilinganishwa na wanaume wakati wa vita, ambapo katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo pekee, kila siku wanawake na wasichana 36 hubakwa, na idadi ya waathirika wa vitendo hivyo ni zaidi ya wanawake laki mbili kutokea mwaka 1998. Hata hivyo, viongozi, vyombo vya upashaji habari, taasisi na mashirika ya kieneo na kimataifa wamekuwa na uzingatiaji mdogo katika masuala hayo. Na hasa ikizingatiwa kwamba, waathirika wa vitendo vya ubakaji wakati wa vita hupatwa na machungu makubwa ikilinganishwa na wa makundi mengine kama yale yanayokabiliwa na mateso ya kimwili na kiakili. Kwa minajili hiyo, mkutano huo unaohudhuriwa na wajumbe kutoka nchi 117 duniani ili kujadili vitendo vya ubakaji wakati wa vita unaonekana kuwa na mguso maalumu. Hakuna shaka kuwa, mikutano kama hiyo itasaidia kufungua njia za kukabiliana na vitendo hivyo, pamoja na kuwazingatia waathirika wa vitendo vya ubakaji kwenye maeneo ya vita. Kuwepo mikakati madhubuti na imara ya kuwafuatilia kisheria watenda jinai hizo sanjari na kuwasaidia waathirika wa vitendo hivyo, kutazuia kuongezeka na kukaririwa mara kwa mara vitendo vya ubakaji kwenye maeneo ya vita.

No comments: