Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, July 6, 2013

Tahadhari juu ya hali mbaya ya watu wa Ghaza

Jumuiya na taasisi mbalimbali za kimataifa zimetoa tahadhari kubwa kuhusu hali mbaya ya wakazi wa eneo la Ukanda wa Ghaza huko Palestina kufuatia kuanza kipindi cha majira ya joto katika pwani ya Bahari ya Meditteranian.
Taarifa iliyotolewa na jumuiya zisizo za serikali za Palestina imesema wakazi wa Ukanda wa Ghaza wanasumbuliwa na uhaba mkubwa wa maji safi na bidhaa muhimu kama dawa na chakula, kutokana na siasa za kidhalimu za utawala wa Kizayuni wa Israel unaendelea kulizingira eneo hilo. Jumuiya hizo zimesisitiza kuwa, mzingiro wa Israel unaoendelea kwa miaka saba mfululizo katika eneo hilo ni sawa na kuwapa mateso ya umma wakazi wote wa Ghaza na ni ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu na sheria za kimataifa.

Hali mbaya ya watu wa Ghaza kutokana na siasa za kidhalimu na kigaidi za Israel katika eneo hilo imefikia kiwango cha tahadhari na inaripoti kuwa wagonjwa wanaolazwa katika hospitali na vituo vya afya ni mbaya sana kutokana na joto kali na ukosefu wa dawa na zana za tiba.
Ukanda wa Ghaza wenye jamii ya watu zaidi ya milioni moja na nusu, unazingirwa na utawala ghasibu wa Israel kwa miaka saba sasa na viongozi wa utawala huo dhalimu wamekuwa wakizuia kuingizwa huko bidhaa na mahitaji muhimu hususan dawa na zana za tiba.
Awali Wakala wa Misaada kwa Wapalestina wa Umoja wa Mataifa UNRWA ulikuwa umetahadharisha juu ya hali mbaya ya wakazi wa Ghaza. Mkurugenzi wa Operesheni za UNRWA Robert Turner ameitaka jamii ya kimataifa kufanya jitihada kubwa za kukomesha mzingiro wa Ghaza.
Maafisa wa UNRWA wanasema eneo la Ukanda wa Ghaza linasumbuliwa na uhaba mkubwa wa dawa na zana za tiba na kwamba akiba ya dawa katika eneo hilo imemalizika.
Mbali ya hayo watu wa Ghaza wanakabiliwa na upungufu mkubwa wa maji safi na iwapo hali hiyo itaendelea watakumbwa na mgogoro mkubwa wa ukosefu wa maji.
Mzingiro wa Israel dhidi ya watu wa Ghaza umewafanya Wapalestina milioni moja na nusu wakose huduma muhimu za kimsingi na kuwatumbukiza wengi wao katika umaskini na ukosefu wa kazi.
Kwa sababu hiyo wafuatiliaji wa mambo wanasisitiza kuwa umewadia wakati kwa walimwengu kukomesha kimya chao mbele ya jinai zinazoendelea kufanywa na utawala haramu wa Israel katika eneo hilo la dunia na kupaza sauti zao kukemea ukatili huo unaofanyika katika karne ya 21 tena kwa msaada na hiyama ya nchi zinazodai zimestaarabika.
Ni kwa sababu hiyo pia ndiyo maana jumuiya mbalimbali za Kipalestina na ile ya UNRWA zikamtaka Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon kukomesha haraka hali mbaya inayowasumbua wakazi wa Ukanda wa Ghaza.

No comments: